• HABARI MPYA

    Monday, April 30, 2018

    YANGA SC KUIFUATA USM ALGER ALHAMISI, MECHI JUMAPILI UFUNGUZI MAKUNDI KOMBE LA SHIRIKSIHO

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    YANGA SC inatarajiwa kuondoka nchini Alhamisi kwenda Algeria kwa ajili ya mchezo wake wa kwanza wa Kundi D Kombe la Shirikisho la Soka Afrika dhidi ya wenyeji, USM Alger mjini Algiers Jumapili.
    Yanga SC imerejea mazoezini leo baada ya jana kuchapwa na mahasimu wao wa jadi, Simba SC 1-0 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. 
    Ofisa Habari wa Yanga SC, Dismass Ten ameiambia Bin Zubeiry Sports – Online leo kwamba kikosi kitaondoka Dar es Salaam Alhamisi kwa ndege ya Emirates Air kikipitia Dubai tayari kwa mchezo huo.
    Pamoja na Yanga na USM Alger, timu nyingine katika Kundi D ni Rayon Sport ya Rwanda na Gor Mahia ya Kenya ambazo zitamenyana zenyewe katika ufunguzi wa hatua ya 16 Bora ya Kombe Shirikisho Afrika.
    Ikumbukwe Kundi A lina timu za ASEC Mimosa ya Ivory Coast, Raja Club Athletic, maarufu Raja Casablanca ya Morocco, AS Vita ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Aduana Stars ya Ghana.
    Kundi B linaundwa na RS Berkane ya Morocco, Al Masry ya Misri, UD Songo ya Msumbiji na El Hilal ya Sudan, wakati Kundi C lina timu za CARA ya Kongo, Enyimba ya Nigeria, Williamsville na Djoliba ya Mali.
    Baada ya mechi ya kwanza ugenini Jumapili, Yanga itamenyana na Rayon Sport mjini Dar es Salaam Mei 16 na itakamilisha mechi za mzunguko wa kwanza kwa kuwafuata Gor Mahia mjini Nairobi Julai 18.
    Mzunguko wa pili Yanga itaanzia nyumbani Julai 29 na Gor Mahia, kabla ya kuwakaribisha na USMA Alger Agosti 19 na kwenda kumalizia ugenini Agosti 29 na Rayon.

    RATIBA YA MECHI ZA YANGA KUNDI D
    Mei 6, 2018: USMA v Yanga, Algiers
    Mei 16, 2018: Yanga v Rayon, Dar Es Salaam
    Julai 18, 2018: Gor Mahia v Yanga, Nairobi 
    MECHI ZA MARUDIANO
    Julai 29, 2018: Yanga v Gor Mahia, Dar es Salaam
    Agosti 19, 2018: Yanga v USMA, Dar es Salaam
    Agosti 29, 2018: Rayon v Yanga, Kigali
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA SC KUIFUATA USM ALGER ALHAMISI, MECHI JUMAPILI UFUNGUZI MAKUNDI KOMBE LA SHIRIKSIHO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top