• HABARI MPYA

    Sunday, September 25, 2016

    YANGA HOI, CHALI KAMBARAGE, WAPIGWA 1-0 NA STAND UNITED

    Na Mwandishi Wetu, SHINYANGA
    MABINGWA watetezi, Yanga SC wamepoteza mchezo wa kwanza wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara baada ya kufungwa bao 1-0 na wenyeji Stand United, Uwanja wa Kambarage, Shinyanga jioni ya leo.
    Shukrani kwake mfungaji wa bao hilo pekee Athanas Pastory na sasa Stand United inafikisha pointi 12 na kupanda hadi nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi, nyuma ya Simba yenye pointi 16.
    Yanga inayobaki na pointi zake 10 baada ya mechi sita, sasa inakwenda kambini Pemba kujiandaa na mchezo dhidi ya mahasimu, Simba SC Oktoba 1, mwaka huu.
    Dakika 45 za kipindi cha kwanza zilimalizika timu hizo zikiwa hazijafungana, zaidi ya kushambuliana kwa zamu.
    Kipindi cha pili, Stand United walikianza vizuri na kufanikiwa kupata bao dakika ya 58 kupitia Pastory Athanas aliyepasua katikati ya mabeki wa Yanga, Vincent Bossou na Mwinyi Hajji Mngwali kwenye boksi kabla ya kumtungua kipa Ally Mustafa Mtinge ‘Barthez’. 
    Kocha Mholanzi Hans van der Pluijm alimtoa kiungo Deus David Kaseke baada ya bao hilo na kumuingiza Juma Mahadhi.
    Mabadiliko hayo hayakuweza kuisaidia Yanga SC kubadilisha matokeo ya mchezo, kwani bao la Pastory lilidumu hadi filimbi ya mwisho. 
    Kikosi cha Stand United kilikuwa; Frank Mwamongo, Revocatus Richard, Adeyum Ahmed, Erick Mulilo, Ibrahim Job, Jacob Masawe, Pastor Athanas, Geremy Katura, Kelvin Sabato, Suleiman Kassim ‘Selembe’ na Adam Kingwande/Abasarim Chidiebere dk86.
    Yanga SC; Ally Mustafa ‘Barthez’, Juma Abdul, Mwinyi Hajji/Haruna Niyonzima dk86, Vincent Bossou, Andrew Vincent, Mbuyu Twite, Simon Msuva, Thabani Kamusoko, Donald Ngoma/Obrey Chirwa dk86, Amissi Tambwe na Deus Kaseke/Juma Mahadhi dk62.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA HOI, CHALI KAMBARAGE, WAPIGWA 1-0 NA STAND UNITED Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top