• HABARI MPYA

    Wednesday, February 11, 2015

    TRA YAMWAGA MILIONI 900 TAIFA STARS, WACHEZAJI SASA ‘WATANUKA FWEZA’

    Na Mahmoud Zubeiry, NAIROBI
    MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) imefikia makubaliano na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kusaini Mkataba wenye thamani ya Sh. Milioni 900 kwa mwaka kwa ajili ya kusaidia timu ya taifa, Taifa Stars.
    Akizungumza na BIN ZUBEIRY mjini hapa jana, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Zuberi Kabwe amesema kwamba alifanikisha mpango wa kuiunganisha TFF na TRA hadi kufunga ndoa hiyo.
    “Wakati wowote Mkataba utasainiwa baina ya TFF na TRA, ambao utainufaisha Taifa Stars kwa kupata Sh. Milioni 900,”amesema Zitto ambaye alikuwa njiani kwenda Mombasa.
    Mheshimiwa Zitto Kabwe kulia amefanikisha mpango wa TRA kuisaidia Taifa Stars

    Mwenyekiti huyo wa Kamati ya Bunge ya Hesabu Za Serikali (PAC), amesema katika Mkataba huo, kiasi cha Sh. Milioni 300 kitakwenda TFF maalum kwa ajili ya shughuli za kiutendaji, wakati Milioni 600 zote zitakuwa kwa ajili ya wachezaji.
    Amesema Milioni 300 moja kwa moja yatakuwa maslahi ya wachezaji wa timu ya taifa ya kwanza na ya pili, maarufu kama Maboresho, wakati Milioni 300 nyingine zitatumika kulipa bima za wachezaji.
    Na akasema TRA yenyewe itanufaika na kutumia picha za wachezaji nyota wa Taifa Stars katika mabango ya kampeni ya ulipaji kodi.
    “Wachezaji nyota wa Taifa Stars kama Mbwana Samatta, Thomas Ulimwengu au Mrisho Ngassa, picha zao zitawekwa kwenye mabango ya TRA nchi nzima wakiwahamasisha watu kudai risiti wanaponunua bidhaa,”amesema.
    Aidha, Zitto Kabwe amesema kwamba amedhamiria zaidi kuisaidia soka ya Tanzania na anaendelea na michakato mbalimbali ya kuusaidia mchezo huo kiuchumi.    
    Zitto ni kati ya wanasiasa vijana nchini wenye mvuto wa kipekee katika jamii, kutokana na harakati zao za kizalendo, zinazomfanya aungwe mkono hata na watu wa chama tawala, CCM japokuwa yeye ni wa chama cha upinzani, CHADEMA.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TRA YAMWAGA MILIONI 900 TAIFA STARS, WACHEZAJI SASA ‘WATANUKA FWEZA’ Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top