• HABARI MPYA

    Wednesday, April 18, 2018

    FAINALI KOMBE LA TFF 2018 KUPIGWA JUNI 2 UWANJA WA SHEIKH AMRI ABEID MJINI ARUSHA

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    FAINALI ya Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), maarufu kama Azam Sports Federation Cup (ASFC) inatarajiwa kuchezwa Juni 2, mwaka huu  Uwanja wa Sheikh Amri Abeid mjini Arusha.
    Taarifa ya TFF kwa vyombo vya Habari leo imesema kwamba katika mashindano ya ASFC mwaka huu kumefanyika maboresho ya kuongeza zawadi na msimu huu mshindi wa pili ambaye awali alikuwa anaambulia mfano wa Medali za Fedha pekee, safari hii atapata Sh. Milioni 10 wakati bingwa ataondoka na kitita cha Sh. Milioni 50.
    Zawadi nyingine zitakazotolewa ni pamoja na Mchezaji bora wa mashindano atakayezawadiwa shilingi milioni Moja, Kipa Bora atapata shilingi Milioni Moja huku mfungaji Bora pia akipata shilingi Milioni Moja wakati mchezaji Bora wa mchezo wa fainali akijizolea shilingi Laki Tano.
    Michuano hiyo imefikia hatua ya Nusu Fainali ambazo zinafanyika wikiendi hii, Stand United wakiwa wenyeji wa Mtibwa Sugar Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga na Singida United wakiikaribisha JKT Tanzania Uwanja wa Namfua.
    Wakati huo huo; Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limeziagiza klabu zote kuwa makini na mikataba wanayoingia na Wachezaji pamoja na makocha wao.
    Taarifa ya TFF leo imesema kwamba haitasita kuzikata fedha klabu zote zitakazokuwa na madeni yanayodaiwa iwe kwa kukiuka mikataba yao na wachezaji, makocha au kwa namna nyingine yoyote.
    “Kumekuwa na klabu zinazolalamika kinyume na utaratibu, tunazitahadharisha kufuata utaratibu unaofahamika, kinyume cha hapo hatutasita kuchukua hatua kali kwa yeyote atakayekiuka utaratibu,”imesema taarifa ya shirikisho hilo.
    TFF imezikumbusha klabu kutoa malalimiko yao kwa njia za kikanuni ili kuepuka hatua ambazo zinaweza kuchukuliwa dhidi yao kama Ibara ya 50 ya katiba ya TFF inavyozungumza pamoja na Kanuni za Maadili.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: FAINALI KOMBE LA TFF 2018 KUPIGWA JUNI 2 UWANJA WA SHEIKH AMRI ABEID MJINI ARUSHA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top