• HABARI MPYA

    Tuesday, March 13, 2018

    TSHISHIMBI AMGARAGAZA OKWI TUZO YA MCHEZAJI BORA WA MWEZI LIGI KUU

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    KIUNGO wa Yanga SC, Papy Kabamba Tshitshimbi amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kwa mwezi Februari, mwaka huu.
    Tshishimbi, raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) aliye katika msimu wake wa kwanza Yanga SC baada ya kusajiliwa kutoka Mbabane Swallows ya Swaziland, ametwaa tuzo hiyo akiwashinda mshambuliaji Mganda wa Simba, Emmanuel Okwi na kiungo mwenzake Jangwani, Pius Buswita. 
    Katika mwezi Februari, Okwi aliongoza kwa kufunga mabao, akifunga mara nne akifuatiwa na Tshishimbi matatu na Buswita mawili.
    Papy Kabamba Tshitshimbi ndiye Mchezaji Bora wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kwa mwezi Februari 

    Lakini Tshishimbi alikuwa ana pasi ya bao pia kwenye mwezi huo na bahati nzuri kwake hakuonyeshwa kadi yoyote, wakati Okwi alionyeshwa kadi ya njano.
    Kingine kilichombeba Tshishimbi kumbwaga Okwi ni kuiwezesha Yanga SC kukusanya pointi 12 Februari, wakati Simba ilivuna pointi 10 tu.
    Kwa ushindi huo,Tshishimbi atazawadiwa fedha taslimu Sh. Milioni 1 kutoka kwa wadhamini wa Ligi hiyo, Kampuni ya Vodacom Tanzania pamoja na kisimbuzi (decoder) kutoka kwa wadhamini wa matangazo wa Ligi hiyo, Azam TV na ngao ya kumbukumbu ya ushindi wake.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: TSHISHIMBI AMGARAGAZA OKWI TUZO YA MCHEZAJI BORA WA MWEZI LIGI KUU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top