• HABARI MPYA

    Wednesday, March 03, 2021

    AZAM FC YAWALAMBA KAGERA SUGAR 2-1 KAITABA, WENYEJI WENGINE WOTE NAO WAPIGWA KWAO LIGI KUU

    TIMU ya Azam FC imeibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya wenyeji, Kagera Sugar katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara leo Uwanja wa Kataba Bukoba.
    Mabao ya Azam FC yamefungwa na kiungo Bryson Raphael dakika ya 20 na mshambuliaji Mzimbabwe, Prince Dube dakika ya 27, wakati la Kagera Sugar limefungwa na Peter Mwalyanzi kwa penalti dakika ya 42.
    Kwa ushindi huo, Azam FC inafikisha pointi 40 baada ya kucheza mechi 22, ingawa inabaki nafasi ya tatu sasa ikizidiwa pointi tano na mabingwa watetezi, Simba SC walio nafasi ya pili japo wana mechi tatu mkononi.
    Vigogo, Yanga SC ambao kesho watakuwa wageni wa Coastal Union Uwanja wa Mkwakwani Jijini Tanga, wanaendelea kuongoza Ligi Kuu kwa pointi zao 49 za mechi 21.
    Dodoma Jiji FC imeibuka na ushindi wa 2-0 ugenini dhidi ya Ruvu Shooting Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani mabao ya Dickson Ambundo dakika ya 35 na Peter Mapunda dakika ya 70.
    Uwanja wa Mwadui Complex, Kishapu mkoani Shinyanga, bao pekee la Nzigamasabo Steve dakika ya 61 limipa Namungo FC ushindi wa 1-0 dhidi ya wenyeji, Mwadui FC.
    Na Uwanja wa Highland Estate juko Ubaruku, Mbarali mkoani Mbeya, Gwambina FC wameibuka na ushindi wa 2-1 dhidi ya wenyeji, Ihefu SC. 
    Mabao ya Gwambina yamefungwa na Rajab Athumani dakika ya 19 na Paul Nonga dakika ya 74, wakati la Ihefu SC limefungwa na Andrew Simchimba dakika ya 90 na ushei.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM FC YAWALAMBA KAGERA SUGAR 2-1 KAITABA, WENYEJI WENGINE WOTE NAO WAPIGWA KWAO LIGI KUU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top