• HABARI MPYA

    Wednesday, May 25, 2016

    YANGA YAITANDIKA AZAM 3-1 NA KUKUSANYA MATAJI YOTE JANGWANI

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    YANGA SC imehitimisha msimu wa 2015/2016 kwa kutwaa mataji yote ya nyumbani, baada ya kuifunga Azam FC mabao 3-1 na kutwaa Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), maarufu kama Kombe la Azam Sports Federation Cup (ASFC) jioni ya leo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Kwa ushindi huo, sasa Yanga ni mbabe asiyepingika wa soka ya Tanzania, baada ya awali kutwaa Ngao ya Jamii Agosti 22, mwaka jana waliposhinda kwa penalti 8-7 dhidi ya Azam FC pia baada ya sare ya 0-0 na mapema mwezi huu kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Katika mchezo wa leo uliochezeshwa na Israel Nkongo, hadi mapumziko, Yanga walikuwa mbele kwa bao 1-0, lililofungwa na mshambuliaji kutoka Burundi, Amissi Joselyn Tambwe dakika ya tisa kwa kichwa akimalizia krosi ya beki wa kulia, Juma Abdul.
    Amissi Tambwe akishangilia baada ya kuifungia Yanga leo Uwanja wa Taifa

    Winga wa Azam FC, Farid Mussa (kulia) akimtoka kiungo wa Yanga, Haruna Niyonzima
    Niyonzima (kulia) akiwania mpira dhidi ya Farid Mussa leo Uwanja wa Taifa

    Yanga ilitawala zaidi mchezo katika kipindi hicho, lakini Azam walifanikiwa kutengeneza nafasi mbili nzuri, ambazo walishindwa kumalizia vizuri.
    Dakika ya pili tu baada ya kuanza kipindi cha pili, Tambwe tena akawafungia Yanga bao la pili, safari hiyo akimalizia krosi ya winga Simon Msuva.
    Mshambuliaji Didier Kavumbangu akaifunga timu yake ya zamani, Yanga SC dakika ya 48 akiujaza mpira nyavuni kwa kifua kumalizia krosi ya winga Ramadhani Singano ‘Messi’.
    Kavumbagu alifunga bao hilo baada ya kuingia kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Nahodha, John Raphael Bocco. 
    Kiungo Deus Kaseke akaifungia Yanga bao la tatu dakika ya 81 kwa shuti kali akimchambua kipa Aishi Manula baada ya kupata pasi ya Msuva.
    Kikosi cha Yanga SC kilikuwa; Deo Munishi ‘Dida’, Juma Abdul, Oscar Fanuel/Mwinyi Mngwali dk58, Kevin Yondan, Vincent Bossou/Nadir Haroub ‘Cannavaro’ dk87, Thaban Kamusoko, Simon Msuva, Haruna Niyonzima/Mbuyu Twite dk65, Donald Ngoma, Amissi Tambwe na Deus Kaseke.
    Azam FC; Aishi Manula, Erasto Nyoni, Gadiel Michael, Aggrey Morris, Abdallah Kheri, Jean Baptiste Mugiraneza, Himid Mao, Mudathir Yahya/Frank Domayo dk63, John Bocco/Didier Kavumbangu dk46, Ramadhani Singano ‘Messi’ na Farid Mussa/Shaaban Iddi dk87.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: YANGA YAITANDIKA AZAM 3-1 NA KUKUSANYA MATAJI YOTE JANGWANI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top