• HABARI MPYA

    Sunday, July 12, 2020

    SIMBA YAWATUPA NJE YANGA AZAM SPORTS FEDERATION CUP, KUKUTANA NA NAMUNGO FANALI SUMBAWANGA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    VIGOGO, Simba SC wametinga Fainali ya michuano ya Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), maarufu kama Azam Sports Federation Cup (ASFC) baada ya kuwachapa watani wao, Yanga SC kwa mabao 4-1.
    Simba SC sasa inakwenda fainali na itakutana na Namungo FC iliyoitoa Sahare All Stars kwa kuichapa 1-0, mchezo ambao utapigwa Agosti 2 Uwanja wa Mandela, Sumbawanga.   
    Mabao ya Simba SC leo yamefungwa na viungo Mbrazil, Gerson Fraga Mzambia, Clatous Chama, Luis Miquissone kutoka Msumbiji na Mzawa Muzamil Yassin.

    Fraga aliifungia bao la kwanza Simba SC kwa shuti kali dakika ya 20 akimalizia krosi ya kiungo Mzambia, Clatous Chama, ambaye alifunga la pili dakika ya 49 akimalizia pasi ya Nahodha John Bocco.
    Miquissone akaifungia bao la pili Simba SC dakika ya 52  akimalizia mpira uliookolewa kwa kichwa na Nahodha wa Yanga SC, Papy Kabamba Tshishimbi baada ya krosi ya kiungo Mkenya, Francis Kahata.
    Yanga SC wakapata bao lao pekee kupitia kwa kiungo wao, Feisal Salum ‘Fei Toto’ dakika ya 70 akimalizia mpira wa adhabu uliopigwa na beki wa kulia, Juma Abdul.
    Kiungo Muzamil Yassin akashindilia msumari wa moto kwenye jeneza la Yanga SC kwa kufunga bao la nne dakika ya 88 akimalizia mpira uliotemwa na kipa Metacha Mnata baada ya shuti la mshambuliaji Mnyarwanda, Meddie Kagere.
    Kikosi cha Simba SC kilikuwa; Aishi Manula, Shomari Kapombe, Mohammed Hussen ‘Tshabalala’, Pascal Wawa, Jonas Mkude, Luis Miquissone/Miraj Athumani 'Madenge' dk89, Gerson Fraga/Muzamil Yassin dk81, John Bocco/Meddie Kagere dk72, Clatous Chama na Francis Kahata/Hassan Dilunga dk71.
    Yanga SC; Metacha Mnata, Juma Abdul, Jaffar Mohamed, Lamine Moro, Said Juma ‘Makapu’, Ppay Kabamba Tshishimbi/Kelvn Yondan dk55, Feisal Salum, Haruna Niyonzima/Ditram Nchimbi dk55, Deus Kaseke, David Molinga na Bernard Morrison/Patrick Sibomana dk64.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA YAWATUPA NJE YANGA AZAM SPORTS FEDERATION CUP, KUKUTANA NA NAMUNGO FANALI SUMBAWANGA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top