• HABARI MPYA

    Friday, February 19, 2016

    SERIKALI: TUNAZUNGUMZA NA TRA WASAMEHE KODI VIFAA VYA MICHEZO

    Na Somoe Ng'itu, DAR ES SALAAM
    WAZIRI Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa Aidha, amesema kwamba ofisi yake inaendelea na mazungumzo na Mamlaka ya Kodi Nchini (TRA) kuhusiana na msamaha wa vifaa vya michezo, lakini itakuwa makini kuhakikisha vifaa vitakavyosamehewa ni vile ambavyo vimeletwa kwa matumizi ya wanamichezo na si wafanyabiashara.
    Waziri Mkuu huyo alisema hayo juzi katika kikao cha pamoja kilichowahusisha pia viongozi wa vyama vya michezo nchini kilichofanyika  kwenye Ukumbi mikutano wa wa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    "Hatuwezi kutoa kodi kwa vifaa vya mtu binafsi, hatutakubali mgongo wa serikali utumike,"alisema Waziri Majaliwa aliyepongeza pia uteuzi wa kocha mkuu mpya wa timu ya Taifa ya soka ya Wanawake (Twiga Stars), Nasra Mohammed na kueleza kwamba hiyo ni hatua nzuri.
    Pamoja na hayo, Waziri Mkuu ameyataka makampuni na taasisi mbalimbali kuidhamini michezo mingine na si kuwekeza nguvu zake kwenye soka pekee.
    Aliwaambia kuwa endapo kila kampuni itajikita kudhamini mchezo mmoja, anaamini mchezo husika utaendelea na kampuni au taasisi hiyo pia itapata nafasi ya kujitangaza kupitia mafanikio ya wanamichezo waliowadhamini.


    Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ameyataka makampuni na taasisi mbalimbali kuidhamini michezo mingine na si kuwekeza nguvu zake kwenye soka pekee

    "Hapa kama kila kampuni moja ikachagua mchezo mmoja na kuudhamini, nina hakika michezo yote ingekuwa inafanya vizuri, hata judo unaweza kukutangaza vizuri, mnatakiwa mpanue wigo," Waziri Mkuu huyo alisema.
    Aliyataka makampuni na taasisi hizo kudhamini kuanzia kwenye ngazi ya wilaya ambayo ndiyo wanamichezo wanaandaliwa na kuacha tabia ya kusubiri timu zinapofika hatua ya kitaifa.
    "Tunawaomba mdhamini vituo na kambi za timu za Taifa, vile vile tunawaomba msaidie kuanzisha vituo," alisema.
    Aliongeza kuwa ili mafanikio yapatikane kwa haraka ni vyema uwekezaji katika kuendesha mafunzo kwa makocha na warefa uimarishwe.
    (Somoe Ng'itu ni mwandishi wa gazeti la Nipashe) 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SERIKALI: TUNAZUNGUMZA NA TRA WASAMEHE KODI VIFAA VYA MICHEZO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top