• HABARI MPYA

    Thursday, June 13, 2013

    YANGA SC WAVUNJA KAMBI NA KUTEMA KOMBE LA KAGAME

    Hawaendi Sudan; Yanga wamevunja kambi kwa wiki mbili
    Na Baraka Kizuguto, IMEWEKWA JUNI 13, 2013 SAA 7:25 MCHANA
    YANGA SC imevunja kambi yake na wachezaji wamepewa mapumziko ya wiki mbili, baada ya Serikali kuzuia timu za Tanzania kwenda Sudan kushiriki Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame.
    Mabingwa hao watetezi wa Kagame mara mbili mfululizo na mara tano jumla, (1975, 1993, 1999, 2011 na 2012) hawatashiriki tena mashindano hayo yanayoandaliwa na Baraza la Vyama Soka Afrika Mashariki Kati  (CECAFA) yaliyopangwa kuanza kutimua vumbi nchini Sudan Jumanne wiki ijayo, Juni 18.
    Yanga haitashiriki mashindano hayo kufuatia kauli ya Serikali juu ya kutozirushu timu zake kwenda kwenye mashindano hayo kutokana na hofu ya usalama kwa wachezaji na viongozi wakati wa mashindano hayo.
    Mapema jana Bungeni, Dodoma, Naibu Waziri wa Habari Utamaduni na Michezo, Amos Makalla alisema hali ya usalama katika miji ya El- Fashir na Kadugli sio nzuri, Serikali haitaziruhusu timu za Tanzania kwenda kushiriki michuano hiyo.
    “Sehemu ambayo mashindano yanafanyika hakuna usalama wa kutosha, mwisho kutembea saa 12 jioni, huduma za hoteli ni duni hazijitoshelezi kuweza kukaa kwa timu katika miji hiyo na kubwa zaidi ni hali ya usalama, kutoka Khartoum mpaka Al Fashir inabidi kutumia usafiri wa Helikopta kitu ambacho bado ni hatari,” alisema Makalla.
    Kocha Mkuu wa Yanga SC, Mholanzi Ernie Brandts amepongaza Serikali kwamba imetazama mbali na kuona umuhimu wa usalama kwa watu wake, kwani hawawezi kucheza michuano zaidi ya wiki mbili katika maeneo yanayolindwa na vikosi vya majeshi ya ulinzi na usalama kutoka nchi mbalimbali.
    Yanga ilianza mazoezi wiki iliyopita Uwanja wa sekondari ya Loyola, Mabibo, Dar es Salaam kujiandaa na mashindano hayo, sasa itajikusanya tena baada ya wiki mbili kuanza maandalizi ya msimu mpya wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Timu nyingine za Tanzania zilizokuwa zicheze michuano hiyo ni Simba SC ya Dar es Salaam na Super Falcon ya Zanzibar.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: YANGA SC WAVUNJA KAMBI NA KUTEMA KOMBE LA KAGAME Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top