• HABARI MPYA

    Friday, March 04, 2022

    SIMBA YAICHAPA BIASHARA UNITED 3-0 MKAPA


    MABINGWA watetezi, Simba SC wamerejea na moto kwenye Ligi Kuu ya Tanzania Bara baada ya kuichapa timu ngumu, Biashara United mabao 3-0 usiku huu Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.
    Mabao ya Simba yamefungwa na winga Msenegal, Pape Ousmane Sakho dakika ya tisa na viungo, Mzawa Muzamil Yassin dakika ya 14 na Mzambia, Clatous Chama dakika ya 18.
    Kwa ushindi huo, Simba SC wanafikisha pointi 34, sasa wakizidiwa nane na watani, Yanga baada ya timu zote kucheza mechi 16, wakati Biashara United inabaki na pointi zake 15 za mechi 16 nafasi ya 14.
    Mechi nyingine ya Ligi Kuu leo, wenyeji, Kagera Sugar wamelazimishwa sare ya 1-1 na Namungo FC Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.
    Kagera Sugar walitangulia kwa bao la Mbaraka Yussuf dakika ya 22, kabla ya Emmanuel Charles kuisawazishia Namungo FC dakika nne baadae.
    Kagera Sugar inafikisha pointi 21 katika mchezo wa 17 ikiwa nafasi ya nane, wakati Namungo FC inafikisha pointi 25 mchezo wa 17 pia, ingawa inabaki nafasi ya nne ikizidiwa tu wastani wa mabao na Azam FC.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA YAICHAPA BIASHARA UNITED 3-0 MKAPA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top