• HABARI MPYA

    Wednesday, November 13, 2013

    MADOGO WAWAADHIRI MAFAZA STARS, WAWAPIGA KIDUDE NA KUWALAZA NACHO

    Na Mahmoud Zubeiry, Ilala
    TIMU ya soka ya pili ya taifa, Future Young Taifa Stars jioni hii imeifunga timu ya kwanza, Taifa Stars bao 1-0 katika mchezo maalum wa kirafiki Uwanja wa Karume, Dar es Salaam.
    Bao pekee la Future limefungwa na mshambuliaji wa Ruvu Shooting ya Pwani, Elias Maguri aliyeunganisha krosi ya chipukizi wa Mtibwa Sugar ya Morogoro, Juma Luizio.
    Kabla ya kutia krosi, Luizio alimpokonya mpira beki mkongwe wa Yanga na mchezaji bora wa Ligi Kuu msimu uliopita, Kevin Yondan ambaye alianzishiwa na kipa wake, Ally Mustafa ‘Barthez’.
    Elias Maguri kulia akipongezana na Juma Luizio baada ya kufunga leo Karume

    Kwa ujumla Future waliihenyesha Stars inayoundwa na wachezaji nyota wa Tanzania wakiwemo Mrisho Ngassa, ambaye hii leo alishindwa kufurukuta.
    Kipa Ivo Mapunda wa Gor Mahia ya Kenya alipewa nafasi kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Barthez lango la Stars na akadaka dakika 45 zote bila kuruhusu bao licha ua Future kushambulia kwa wingi.
    Deo Munishi ‘Dida’ wa Yanga alianza katika lango la Future na kipindi cha pili akampisha Aishi Manula  wa Azam FC ambaye pia alifanya kazi nzuri.
    Baada ya mechi, kocha wa Stars, Mdenmark Kim Poulsen alisema amevutiwa na uwezo wa kipa Mapunda na kwa ujumla mechi hiyo imemsaidia katika mkakati wake wa kuunda kikosi imara cha kudumu cha timu yake.
    Rais mpya wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi alikuwepo Uwanja wa Karume na baada ya mechi alizungumza na wachezaji akiwataka wafanye kazi nzuri ili wafurahie matunda ya uongozi wake.
    Akawaambia Novemba 19 watacheza na Kenya, Harambee Stars, mchezo wa kirafiki Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.  
    Future imeweka kambi hoteli ya Sapphire, wakati Stars ipo kambini Tansoma Hotel, zote maeneo ya Kariakoo, Dar es Salaam.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MADOGO WAWAADHIRI MAFAZA STARS, WAWAPIGA KIDUDE NA KUWALAZA NACHO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top