Mungu ibariki Taifa Stars |
SHIRIKISHO la Soka la Kimataifa (FIFA) limeteua waamuzi kutoka Algeria kuchezesha mechi kati ya Taifa Stars na Ivory Coast itakayofanyika Jumapili saa 9:00 Alasiri kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Waamuzi hao watakaochezesha mechi hiyo ya kundi C kuwania tiketi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia mwakani nchini Brazil wataongozwa na Charef Mehdi Abid atakayepuliza filimbi. Atasaidiwa na Hamza Hammou na Bouabdallah Omari wakati mezani atakuwa Sofiane Bousseter.
Abdi na wezake wanatarajiwa kutua nchini Ijumaa (Juni 14 mwaka huu) saa 12 asubuhi kwa ndege ya Shirika la Usafiri wa Anga la Misri. Mtathmini wa waamuzi ni Athanase Nkubito kutoka Rwanda ambaye atatua nchini Ijumaa (Juni 14 mwaka huu) saa 12 jioni kwa ndege ya RwandAir.
Kamisaa wa mechi hiyo ni Bernard Mfubusa kutoka nchini Burundi ambapo atawasili nchini Ijumaa (Juni 14 mwaka huu) saa 3.35 asubuhi kwa ndege ya Kenya Airways. Maofisa wote hao wa mechi hiyo watarejea makwao Jumatatu (Juni 17 mwaka huu).
Wakati Ivory Coast iliifunga Gambia 3-0 Jumamosi, Stars ilifungwa 2-1 na wenyeji Jumamosi katika michezo iliyopita ya Kundi C kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Kombe la Dunia Brazil mwakani.
Stars ipo nafasi ya pili mbele ya Morocco yene pointi tano sasa, wakati Ivory Coast wanaongoza kwa pointi zao 10, zikiwa zimesalia mechi mbili mbili kumaliza hatua ya makundi.