Nsa aliyebinuka tik tak mbele ya Juma Nyosso wa Simba, enzi hizo akiichezea Yanga. Leo atawafunga kweli Simba? |
Na Mahmoud Zubeiry, Tanga
NSA Job, mshasmbuliaji wa Coastal
Union ya Tanga amesema kwamba hakuna beki wa Simba anayeweza kumzuia asifunge
bao katika mechi ya leo, kwa sababu wote anawajua.
Nsa amewaahidi raha mashabiki wa
Coastal Union leo, akisema kwamba dakika 90 ni nyingi mno kwake na haziwezi
kumalizika bila kufunga hata bao moja.
“Nawaahidi wapenzi na mashabiki wa
Coastal furaha katika mechi yetu na Simba, nitawafunga lazima, kwa sababu
hakuna beki wa kunizuia mimi kufanya hivyo, sijui wawe na bahati gani tu
niwakose,”alisema Nsa.
Nsa alisema kwamba kwa ujumla timu
yao iko vizuri na nia yao msimu huu ni kufanya vizuri katika Ligi Kuu ili
kuwakumbusha wakazi wa Tanga, enzi za Coastal iliyokuwa tishio katika soka ya
Tanzania.
“Simu ni timu ya kawaida sana,
tunaijua vizuri, hakuna kipya pale na kwa kudhihirisha hilo, sisi tunawafunga kwenye
mechi hii,”alisema Nsa.
Nsa amewahi kucheza Simba msimu wa
2006, lakini akatemwa na kurejea Moro United kabla ya baadaye kusajiliwa Azam
FC, Yanga, Villa Squad na msimu huu ametua Tanga.