• HABARI MPYA

    Sunday, October 28, 2012

    HAPA NDIPO AZAM ILIPOJKWAA JANA MBELE YA SIMBA

    John Bocco akiwa chini ya benchi la Azam baada ya kuumia.

    ILITARAJIWA kuwa mechi ngumu na hata ilivyoanza ilionekana itakuwa mechi ngumu, lakini ndani ya dakika 22 mwelekeo mzima ukabadilika.
    Na Mahmoud Zubeiry
    Naizungumzia mechi ya jana ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, baina ya mabingwa watetezi, Simba SC dhidi ya washindi wa pili wa ligi hiyo msimu uliopita, Azam FC.  
    Katika mechi hiyo, iliyopigwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Simba ilitoka nyuma kwa bao 1-0 na kushinda 3-1.
    Ushindi huo, unaifanya Simba izidi kujitanua kileleni mwa ligi hiyo kwa kufikisha pointi 22, baada ya kucheza mechi 10, wakati Azam FC inapromoka hadi nafasi ya tatu kwa pointi zake 18, baada ya kucheza mechi tisa, ikiipisha Yanga nafasi ya pili, ambayo imetimiza pointi 20 baada ya kuifunga JKT Oljoro jana.
    Mabao ya Simba jana yalitiwa kimiani na Emanuel Arnold Okwi mawili na Felix Mumba Sunzu Jr. moja, wakati la Azam lilifungwa na John Raphael Bocco ‘Adebayor’.
    Hadi mapumziko, tayari Simba walikuwa mbele kwa mabao 2-1, Azam wakitangulia kufunga dakika ya nne, kupitia kwa Adebayor ambaye alimtoka beki Mkenya Paschal Ochieng na kumchambua Juma Kaseja.
    Dakika mbili baadaye, Sunzu aliisawazishia Simba, akiunganisha kwa kichwa krosi maridadi ya Mrisho Khalfan Ngassa kutoka wingi ya kulia.
    Okwi aliifungia Simba bao la pili kwa kichwa dakika ya 40, baada ya kutokea kizaazaa langoni mwa Azam kufuatia mpira uliopigwa langoni mwa timu hiyo na Mwinyi Kazimoto.    
    Kipindi cha pili Simba walirudi na moto wao na iliwachukua dakika tano tu kuhitimisha karamu yao ya mabao, baada ya Okwi kuwainua tena vitini mashabiki wa Simba, akifumua shuti la umbali wa mita 19, baada ya kuwatoka mabeki wa Azam.
    Mrisho Ngassa ndiye alikuwa nyota wa mchezo wa jana, kutokana na kuisumbua mno Azam, iliyomuuza kwa mkopo Simba miezi miwili iliyopita.
    Kulingana na kuporomoka kwa kiwango cha soka yetu, kwa sasa mechi za uhakika zilizobaki ambazo unaweza kuziita za ushindani ni kati ya Simba na Azam, Simba na Yanga na Yanga na Azam.
    Zipo timu nyingine ambazo zinaleta ushindani, lakini si wa uhakika sana- ila Azam, hakika imeleta changamoto mpya katika soka ya Tanzania.
    Mechi ya jana Simba walishinda kwa urahisi pengine tofauti kabisa na wao walivyotarajia. Simba walitarajia ugumu mno kwenye mechi hiyo hata wakaamua kwenda kuweka kambi Zanzibar kujiandaa vizuri.
    Waliipa mechi hiyo uzito wa mechi zao na Yanga ndiyo maana wakaenda Zanzibar, ambako tumezoea kusikia Simba ikienda katikati ya Ligi, basi kwa ajili ya kucheza na wapinzani wao hao wa jadi.
    Kwa nini mechi ilikuwa nyepesi ghafla?
    Mfungaji wa bao la kwanza katika mechi hiyo, John Bocco ‘Adebayor’ aliumia dakika ya 20 na jitihada za kumtibu kwa dakika nne zilishindikana hatimaye akatoka na nafasi yake ikachukuliwa na kiungo Khamis Mcha ‘Vialli’ dakika ya 25.
    Hapo ndipo mechi ilipobadilika kabisa, kwa sababu kuanzia hapo Azam ilicheza bila mshambuliaji uwanjani.
    Sijui kwa sababu gani kocha Mserbia wa Azam, Boris Bunjak na wasaidizi wake walishindwa kuingiza mshambuliaji mwingine baada ya kuumia Bocco na badala yake wakaingiza kiungo, wakati kwenye benchi alikuwepo Gaudence Exavery Mwaikimba.
    Nasema sijui kwa sababu, Bunjak na wasaidizi wake ndiyo wana siri ya timu yao, nani alikuwa katika hali gani, maana habari zilizopatikana jana zinasema hata Bocco alicheza akiwa ana maumivu na kilichotokea jana alitoneshwa tu hadi akatoka.
    Bocco akimgeuza Ochieng
    Nachotaka kuzungumzia leo ni kwa nini mechi iliyotarajiwa kuwa ngumu ikawa nyepesi mno- Azam kucheza bila mshambuliaji kuanzia dakika ya 20 ndiko kuliwapa ahueni Simba kwenye mchezo huo.
    Wakati Bocco alipokuwa uwanjani, mabeki wa Simba walikuwa hawaendi juu ili kumchunga hasa baada ya kuwafunga bao la kwanza na zaidi hata viungo wakabaji, Jonas Mkude na Amri Kiemba nao walikuwa wanakwenda juu kwa machale sana.
    Hiyo iliwapa fursa kwa Azam kufanya mashambulizi zaidi langoni mwa Simba na kukosa mabao kadhaa hata wakati timu hizo zikiwa 1-1.
    Wakati Azam inaongoza 1-0, waliruhusu bao la kusawazisha kwa makosa ya kawaida ya kimchezo na zaidi hata kipa Mwadini Ali jana hakuwa vizuri, maana hakuwa na jitihada za ziada za kuiokoa timu yake na alikubali kufungwa kiurahisi.
    Lakini baada ya Simba kuona kosa lililofanywa na Azam kufuatia kuumia kwa Bocco, wakawa huru na kushambulia kwa mapana marefu zaidi zaidi.
    Utaona hata Shomary Kapombe na Paschal Ochieng walikuwa wanapanda pia, wabaki nyuma kumlinda nani na wapinzani hawana mshambuliaji?
    Si kama Azam walizidiwa mchezo hapana, bali walidhibitiwa na Simba kwa sababu hawakuwa na mchezaji hatari pale mbele. Kipre Tcheche ni mzuri kweli, lakini ana aina ya mipira yake, muwekee kwenye njia akimbize, mwisho wa siku atoe krosi, nani ataunganisha?
    Krosi nzuri ziliendelea kutiwa kwenye lango la Simba na hata kona, lakini nani angeunganisha? Nani angewatia misukosuko mabeki wa Simba?
    Bunjak amekuwa akimtumia sana kiungo Abdulhalim Humud katika mashambulizi yanayotokana na mipira ya kona, lakini jana alidhibitiwa na kwa sababu Bocco hakuwapo, ilikuwa kazi rahisi mno.
    Si dhambi Azam kufungwa na Simba, lakini inasikitisha mechi iliyotarajiwa kuwa burudani zaidi, inakuwa ya kawaida sana, ukizingatia ligi yenyewe ina mechi chache tu za kutazama.
    Upande wa pili, kwa kuwa Azam watashiriki Kombe la Shirikisho Afrika mwakani, mechi ngumu kama hizi, dhidi ya Simba na Yanga ndio kipimo kwao cha kuujua ubora wa timu yao.
    Sawa, Erasto Nyoni hakuwapo jana na badala yake akacheza Samir Hajji Nuhu, sioni tofauti sana baina ya wachezaji hao, labda uzoefu tu, lakini Mrisho Ngassa angeendelea kuwa hatari tu kwa Azam hata angekuwepo nani
    Azam inahitaji kurudia orodha ya wachezaji iliyowasajili na kisha ijiulize ina washambuliaji wangapi kikosini na wangapi wako tayari kucheza.
    Mshambuliaji ni mshambuliaji tu, ana maarifa ya kupambana na mabeki hasa kwenye mipira inayoelekezwa langoni kutoka pembeni mwa Uwanja. Mshambuliaji anaongeza ladha ya timu kwa kiasi kikubwa sana.
    Na ndiyo maana huyo ndiye mchezaji anayenunuliwa kwa bei mbaya zaidi katika soko la wachezaji duniani.
    Abdi Kassim ‘Babbi’ ana mwili mkubwa, lakini huyu bado ni kiungo tu. Kama Azam haina mshambuliaji zaidi ya Bocco, lawama haziwezi kuwa za Bunjak kwa sababu siye aliyesajili timu.
    Lakini kwa Azam haitakuwa busara kutafuta mchawi kwa sasa, nawaambia watumie mechi hizi dhidi ya Simba na Yanga kuiangalia timu yao kuelekea mwakani katika Kombe la Shirikisho.
    Hii ni timu ambayo ujio wake ulipokewa kama mwanzo wa mapinduzi katika soka ya Tanzania, na kweli dalili tunaziona, ila itapendeza mapinduzi yasiwe tu ya rasilimali, bali na soka pia uwanjani na matokeo mazuri.
    Hivyo, wamalizie mechi za mzunguko wa kwanza huku wakikitathmini kikosi chao na kufikiria namna ya kukiboresha katika usajili wa dirisha dogo ambao utakuwa wa mwisho kuelekea michuano ya Afrika.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: HAPA NDIPO AZAM ILIPOJKWAA JANA MBELE YA SIMBA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top