• HABARI MPYA

    Thursday, February 07, 2019

    BIASHARA UTD INAFANYA BIASHARA GANI, ISO FAIDA WALA HASARA?

    Na Frederick Daudi,  DAR ES SALAAM
    MARA ni miongoni mwa mikoa yenye mafanikio kedekede kwenye nyanja anuai. Huu ndio mkoa uliojaaliwa makabila mengi zaidi nchini hivyo kuna vipaji na vipawa vya kila aina. Kila kabila linafanya vizuri kwenye sekta yake.
    Lakini katika michezo, hususan kwenye soka, ni nani aliyewaroga? 
    Kwa miaka ya nyuma, mkoa huu umekuwa ukiwakilishwa na Polisi Mara kwenye ligi kuu bara. Polisi ambayo nayo imekuwa ikisuasua, hatimaye ilikuja kupotea kabisa kwenye ramani ya ligi hii kubwa zaidi nchini.
    Timu zingine kama Saragire FC na JKT Rwamkoma, kwa nyakati tofauti tofauti ziliwawakilisha akina 'mura' kwenye ligi daraja la kwanza lakini kupanda ligi kuu ikawa ni kizungumkuti.

    Baada ya miaka takribani 15 kupita, hatimaye neema imerudi tena uwanja wa Karume Musoma. Baada ya uwanja huo kuwa mwenyeji wa matamasha kama Fiesta na kampeni za siasa tangu mara ya mwisho Polisi Mara ilipocheza ligi kuu mwaka 2003, sasa shangwe zimerejea tena.
    Safari hii si wengine bali ni Biashara united. Hii ni timu iliyoleta mapinduzi ya Soka kwenye mkoa huu ambao ndio kwao mwasisi wa taifa hili hayati Mwalimu Julius K. Nyerere. Nadhani mzee Nyerere angekwepo, angekuwa shabiki namba moja wa timu Biashara.
    Pamoja na watu wengine, kuna mtu mmoja aliyefanya kazi kubwa mpaka kuifikisha timu hapa. Huyu ni mtu fulani hivi asiye na maneno mengi bali vitendo na mikakati kabambe. Amani Josiah. Mtu asiyefahamika kwa wengi lakini kwa mchango wake kwa Biashara, tunarudi palepale kwamba mnyonge tutamnyonga lakini haki yake tunampa kiroho safi kabisa.
    Baada ya timu kupanda daraja, ikaanza kuwekwa mikakati ya kuifanya timu ifanye vizuri. Mmoja wapo wa mikakati hiyo, ni kuufanya uwanja wa Karume kuwa machinjio ya timu yoyote inayotoka mkoani.
    Katika mechi ya kwanza iliyochezwa Namfua dhidi ya Singida united, tayari Biashara ilianza kuonesha Cheche. Pointi 3 za kwanza katika mechi ya kwanza, uwanja wa ugenini dhidi ya timu yenye uzoefu na ligi, siyo lelemama.
    Sekunde zikapita, dakika zikafuatia, siku zikakatika na sasa miezi kadhaa imepita. Sasa hivi Biashara imecheza mechi 23 ina pointi 20 katika nafasi ya 19.
    Je, nini kimetokea hapo katikati? Baada ya kuwa na mwendelezo mbaya,  hatimaye Biashara iliamua kumleta kocha mpya Amri Said. Kocha huyu aliyekuwa tegemeo la wengi, ameisaidia Biashara kujizolea pointi kadhaa hasa katika uwanja wa nyumbani na kuwapandisha kutoka kuburuza mkia mpaka nafasi ya 18.
    Lakini mbona bado timu haifanyi vizuri? Amani Josiah, aliyekuwa meneja wa timu, alipoona mambo yanaenda kombo, aliamua kukaa pembeni ili kuepusha msongamano. Lakini mbona bado hakueleweki? Kila kukicha afadhali ya juzi na jana.
    Baada ya kuondolewa na Yanga kwenye michuano ya FA, huku kocha akilumbana na kipa Nurdin Balora baada ya kumtoa nje, mambo yamezidi kuwa mabaya. Biashara haifungwi magoli mengi lakini Biashara inapoteza alama nyingi.
    Kwani kuna biashara gani inaendelea huko? Mbona kikosi ni kizuri tu na kocha hana tatizo?
    Ndipo nikagundua kwamba kuna baadhi ya wanaojiita wadau na watu wenye mahaba na bashara, wanaleta chokochoko pale. Kuna siasa na majungu vinaendelea kuiharibu timu. 
    Kama Biashara itashuka daraja, lawama hazitaenda kwa yeyote bali wadau wa soka mkoani Mara. Watu wenye maneno bila vitendo. Watu wanaojitokeza timu ikifanya vizuri na kuingia mitini katika nyakati ngumu. Watu wanaojua kuwalaumu viongozi, kocha na wachezaji lakini wao hawana mchango wowote. 
    Kwa sasa, Biashara united inatakiwa kutulia na kuondoa tofauti zao. Timu ipewe ushirikiano ili ipambane ibaki kwenye ligi. Masuala ya kiongozi gani kafanya nini yatajadiliwa baada ya ligi kumalizika. Kwa ujumla Biashara hawatakiwi kufanya biashara yoyote kwa sasa tofauti na kusakata kabumbu. Tofauti na hapo, kaburi la kushuka daraja litawameza na hatimaye mkoa wa Mara utaendelea kuzishabikia timu kongwe za Kariakoo .
    (Federick Daudi ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) KItovi Uandishi wa Habari na Mawasilaoin y` Umma, ambaye anapatikana kwa barua pepe defederico131@gmail.com na simu namba 0742164329)
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BIASHARA UTD INAFANYA BIASHARA GANI, ISO FAIDA WALA HASARA? Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top