• HABARI MPYA

    Tuesday, June 20, 2023

    MASHABIKI KUINGIA BURE KESHOKUTWA SOKOINE MBEYA CITY NA MASHUJAA


    MKUU wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera amesema mashabiki wataingia bure Uwanja wa Sokoine keshokutwa kwenye mchezo wa marudiano wa mchujo wa kuwania kucheza Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara baina ya Mbeya City na Mashujaa ya Kigoma.
    Homera amesema lengo la kuruhusu watu waingie bure ni kutaka wana Mbeya wajitokeze kwa wingi kuisapoti Mbeya City iweze kupindua matokeo ya kufungwa 3-1 na kubaki Ligi Kuu.
    Wenyeji, Mashujaa jana waliibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Mbeya City katika mchezo wa kwanza wa mchujo wa kuwania kupanda Ligi Kuu Uwanja wa Lake Tanganyika mjini Kigoma.
    Mabao ya Mashujaa yalifungwa na Abihud Mtumbuka dakika ya 24, Asanga Stallone dakika ya 69 na Shadrack Ntabindi kwa penalti dakika ya 78, wakati la Mbeya City alijifunga Aziz Sibo dakika ya 63.
    Timu hizo zitarudiana Alhamisi Uwanja wa Sokoine Jijini Mbeya na Mbeya City itatakiwa kushinda 2-0 ili kufuzu kwa sheria ya mabao ya ugenini.
    Mshindi wa jumla atapanda Ligi Kuu na timu itakayofungwa itakwenda kucheza Ligi ya Championship. Ikumbukwe Mashujaa inacheza mchujo huu ikitoka Championship na Mbeya City imetoka Ligi Kuu.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MASHABIKI KUINGIA BURE KESHOKUTWA SOKOINE MBEYA CITY NA MASHUJAA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top