• HABARI MPYA

    Thursday, June 02, 2016

    AZAM ACADEMY YAANZA VYEMA MICHUANO YA VIJANA AFRIKA MASHARIKI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    TIMU ya vijana ya Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati Azam FC (Azam Academy) jana imeanza vema michuano ya Azam Youth Cup 2016 baada ya kuinyuka Future Stars Academy kutoka Arusha kwa mabao 4-1.
    Mchezo huo uliofanyika jioni ndio ulikuwa wa ufunguzi wa michuano hiyo inayofanyika kwenye Uwanja wa Azam Complex Chamazi, kabla ya kushuhudiwa Ligi Ndogo Academy kutoka nchini Kenya wakiwachapa Football for Good Academy (Uganda) mabao 2-1.
    Azam Academy iliuanza vema mchezo huo kwa kuonyesha uhai mkubwa kipindi cha kwanza na ndani ya dakika 37 tu ikaweza kujipatia mabao yote manne kabla ya Future Stars kuwabana kipindi cha pili kwa kuwazuia wapinzani wao wasipate mabao zaidi.




    Iliwachukua dakika 17 tu, Azam Academy kuweza kupata bao la uongozi lililofungwa na Shaaban Idd aliyemtoka kipa wa Furure Stars, Elias Lembris, kabla ya kufunga bao hilo, dakika moja baadaye Rajabu Odasi akaongeza bao la pili.
    Future Stars ilikuja juu mara baada ya kupata bao la kwanza dakika 25 lililofungwa na Nazir Abdul kwa kichwa, lakini nguvu zao zilinyong’onyeshwa kufuatia Shaaban tena kuipatia bao la tatu Azam Academy dakika ya 28 akitumia vema pasi safi ya nahodha Abdallah Masoud ‘Cabaye’.
    Odasi aliyekuwa kwenye kiwango bora kabisa katika eneo la kiungo akishirikiana vema na Masoud, alipigilia msumari wa mwisho kwenye lango la Future Stars kwa kuipatia bao la nne Azam Academy kwa shuti zuri akiunganisha krosi iliyochongwa na Ramadhan Mohamed.
    Hadi kipindi cha kwanza kinamalizika Azam Academy ilienda kifua mbele kwa mabao hayo, hata iliporejea kipindi cha pili ilishindwa kuongeza mabao mengine kufuatia Future Stars kuubana uwanja.
    Hata hivyo kipa wa Future Stars Elias, anastahili pongezi kubwa kufuatia kuokoa michomo mingi ya wapinzani wao kipindi cha pili, baadhi ikipigwa na Optatus Lupekenya dakika ya 62 na Yahaya Zaidi dakika ya 72.
    Kikosi hicho kinachonolewa na Tom Legg kutoka nchini Uingereza na Msaidizi wake, Idd Cheche kilimaliza mchezo huo kwa ushindi huo mnono na kufanya wafikishe jumla ya pointi tatu wakiwa juu ya Ligi Ndogo ambao walipata ushindi finyu wa mabao 2-1 dhidi ya Football for Good.
    Mchezo huo wa pili ulikuwa mkali na wa aina yake kwa timu zote kugawana vipindi, Football for Good wakimiliki kipindi cha kwanza na Ligi Ndogo waking’ara zaidi kipindi cha pili. Ligi Ndogo ilibidi itoke nyuma baada ya kutanguliwa kufungwa bao dakika ya 39 na Otim Oradiga na kurejea mchezo kwa mabao mawili ya ushindi yaliyopigwa na Eric Kivuva.
    Michuano hiyo kesho itaingia kwenye mapumziko na itaendelea tena keshokutwa Ijumaa, mchezo wa kwanza utakaoanza saa 10.00 jioni utakuwa kati ya Future Stars na Ligi Ndogo huku Azam Academy ikimenyana na Football for Good saa 1.00 usiku.
    Kikosi cha Azam Academy kilikuwa; Metacha Mnata/Kauju Agustino dk 79, Abdul Omary, Ramadhan Mohamed, Abas Kapombe, Adolph Mtasigwa/Joshua John dk 72, Prosper Mushi, Optatus Lupekenya/Sadalla Mohamed dk 65, Masoud Abdallah, Shaaban Idd/Kolongo Idd dk 90, Rajabu Odas, Fereji Salum/Yahaya Zaidi dk 53
    Future Stars: Elias Lembris, Hamdu Harun/Hamadi Aziz dk 58, Baraka Fredy, Saimon Moses, Wazir Abdul, Mahmudu Said, Ally Yusuph, Ahmed Seleman, Ndwiga Roothaert/Khairailah Juma dk 46, Ramadhan Soloka, Hatibu Yassin.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM ACADEMY YAANZA VYEMA MICHUANO YA VIJANA AFRIKA MASHARIKI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top