• HABARI MPYA

    Friday, June 24, 2016

    MBEYA CITY YAMSAJILI MKALI WA MABAO WA PRISONS

    Na David Nyembe, MBEYA
    KLABU ya Mbeya City FC imebomoa ngome ya wapinzani wa Jiji la Mbeya, Prison FC baada ya kufanikiwa kumsajili mshambuliaji wao tegemeo la mabao, Mohamed Mkopi.
    Mbeya City FC leo imemsainisha Mkataba wa mwaka mmoja Mkopi, aliyekuwa pacha wa Jeremiah Juma katika safu ya ushambuliaji ya Prisons katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara msimu uliopita.
    Mkopi, aliyewahi kuchezea pia Mtibwa Sugar ya Manungu, Turiani, mkoani Morogoro amesema kwamba kutua kwake Mbeya City ni kutimia kwa ndoto zake.
    "Ninamshukuru Mungu kwa kufanikiwa kujiunga na City, timu ambayo nilikuwa na ndoto za kuichezea hata kabla ya kusajiliwa na Prison msimu uliopita,"amesema.
    Mohammed Mkopi akisaini Mkataba wa mwaka mmoja kujiunga na Mbeya City kwa mahasimu, Prisons

    “Kabla sijasajiliwa na Prison ndoto yangu ilikuwa ni kucheza kwenye timu hii, nashukuru Mungu baada ya msimu mmoja hili limefanikiwa, nitakuwa hapa msimu ujao, lengo langu ni kufanya kazi kwa nguvu  ili niendelee kuwa sehemu ya kikosi hiki kwa muda mrefu zaidi” amesema.
    Na mpango huu unafanikiwa siku moja tu, baada ya Mbeya City kusaini Mkataba mpya wa kuendelea kudhaminiwa na kampuni ya Bin Slum Tyres Limited, kupitia betri za za RB.
    Katika hafla maalum fupi iliyofanyika kwenye ofisi za Bin Slum Tyres Limited, Lumumba, Dar es Salaam jana machana, Mkurugenzi wa Bin Slum Tyres Limited, Mohammed Bin Slum alisema kwamba wameamua kuiongezea Mkataba klabu hiyo baada ya kuridhishwa na mwenendo wa timu hiyo.
    Mohammed, kiungo wa zamani wa Coastal Union ya Tanga alisema Mkataba mpya na utakuwa na thamani sawa na Mkataba wa awali.
    Naibu Mkurugenzi wa Bin Slum Tyres Limited, Mohammed Bin Slum (kushoto) akitiliana saini mikataba na Meya wa Manispaa ya Mbeya, David Polela Mwashilindi (kulia) jana mjini Dar es Salaam 
    “Tunayo furaha kuongeza Mkataba na Mbeya City baada ya ule wa awali kumalizika na tumefanya hivi baada ya kuvutiwa na mwenendo wao mzima,”alisema Bin Slum.
    Bin Slum Tyres Limited iliingia Mkataba na Mbeya City kwa mara ya kwanza mwaka 2014 ikiwapa dau la Sh. Milioni 360, yaani Sh. Milioni 180 kwa mwaka.
    Fedha hizo ni nje ya vifaa vya michezo wanavyopewa kila mwaka, ambavyo ni pamoja na seti tatu za jezi za kisasa kila msimu. Na mwaka jana Bin Slum Tyres Limited iliwakabidhi Mbeya City basi jipya kubwa la kisasa lenye thamani ya zaidi ya Sh. Milioni 200.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MBEYA CITY YAMSAJILI MKALI WA MABAO WA PRISONS Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top