Mwali; Ametelekezwa |
Na Mahmoud Zubeiry
SIMBA SC wamemtelekeza mwali, sasa Azam FC na Yanga SC ‘wanatoana roho’ kumgombea, nani atashinda vita hiyo?
Kwa kiasi kikubwa ni Watoto wa Jangwani, Yanga SC waliopo kileleni kwa pointi zao 49, wakiizidi Azam FC kwa pointi sita.
Lakini kwa nini usiitilie shaka Yanga kama inaweza kumbeba mwali, ikiwa mwenendo wake wa siku za karibuni katika Ligi Kuu ni wa kujikongoja?
Mechi iliyopita dhidi ya Polisi Morogoro Yanga ililazimishwa sare ya bila kufungana na Maafande hao, wakati mechi tatu zilizotangulia iliibuka na ushindi mwembamba wa bao 1-0 kila mechi dhidi ya Azam, Kagera Sugar, Toto African na Ruvu Shooting.
Ina maana, Yanga ikifungwa mechi mbili zijazo kati ya mechi zake tano, Azam FC inaweza kuwa bingwa. Na Yanga wana mechi ngumu kati ya hizo tano zilizobaki ambazo zinaweza kutoa matokeo yoyote.
Kinachoweza kuzungumzwa hapa; ubingwa bado hauna mwenyewe na ni mbio za farasi wawili, wa Chamazi na Jangwani na sana mfalme mpya wa Ligi Kuu akiwahi kutokea, anaweza kupatikana kuelekea mechi mbili za mwisho za msimu.
Na kwa hesabu hizi, Simba SC imejitoa kabisa katika ramani ya Afrika mwakani- kwani atakayekosa ubingwa ndiye atakayecheza Kombe la Shirikisho na bingwa atakwenda Ligi ya Mabingwa.
Tunaanza kushuhudia ligi yenye taswira tofauti, yenye ushindani na si ligi ile ile tuliyoizoea ya Simba na Yanga tu kushika nafasi mbili za juu.
Msimu uliopita Yanga alikaa benchi wakaenda Simba SC na Azam. Tayari dalili zinaonekana, msimu huu Simba itakaa benchi na Yanga atakwenda na Azam.