• HABARI MPYA

    Friday, June 03, 2016

    ULIMWENGU HATIHATI KUWAVAA MAFARAO KESHO

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI wa TP Mazembe ya DRC, Thomas Emmanuel Ulimwengu 'Rambo' jana hakufanya mazoezi na timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars kwa sababu ya maumivu ya mguu.
    Ulimwengu baada ya kuwasili na wachezaji wenzake Uwanja wa Taifa, alijaribu kufanya mazoezi ya awali ya kuamsha misuli kidogo, kabla ya kushindwa kuendelea na kutoka nje.
    Madaktari wa Taifa Stars walijaribu kuhangaika naye kumrejesha uwanjani, lakini hakuweza kabisa kurudi mazoezini.
    Daktari Mkuu wa Taifa Stars, Gilbert Kigadye akasema Ulimwengu aliumia juzi Taifa Stars na jana ameshindwa kabisa kufanya mazoezi.
    Thomas Ulimwengu akiwa ameketi nje Uwanja wa Taifa jana kushuhudia wenzake wakifanya mazoezi, huku yeye akipatiwa tiba na Madaktari wa Taifa Stars


    “Tunachofanya hapa ni kumpatia tiba ya kuondoa maumivu na kumpumzisha ili pate ahueni. Si maumivu makubwa, aligongwa kidogo tu,”alisema Dk Kigadye.
    Taifa Stars inatarajiwa kumenyana na Misri kesho Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam katika mchezo wa Kundi G kufuzu Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika.  
    Katika mchezo wa kesho, Stars inahitaji ushindi ili kufufua matumaini ya kwenda AFCON ya mwakani.
    Tanzania inashika mkia katika Kundi G, baada ya kucheza mechi mbili, ikifungwa moja ugenini na Misri 3-0 na kutoa sare moja ya 0-0 na Nigeria nyumbani.
    Misri inaongoza kundi hilo kwa pointi zake saba baada ya kucheza mechi tatu sawa na Nigeria yenye pointi mbili.
    Zote, Misri na Nigeria zimebakiza mchezo mmoja mmoja, wakati Tanzania ina mechi mbili – kwanza Jumamosi na Misri nyumbani na baadaye Septemba na Nigeria ugenini.
    Iwapo Tanzania itashinda mechi zote mbili za mwisho watamaliza na pointi saba sawa na Misri, hivyo timu ya kufuzu AFCON ya mwakani kutoka Kundi G kupatikana kwa wastani wa mabao.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ULIMWENGU HATIHATI KUWAVAA MAFARAO KESHO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top