• HABARI MPYA

    Sunday, January 25, 2015

    OKWI AZIMIA BAADA YA KUIFUNGIA BAO SIMBA IKITOKA SARE NA AZAM, AKIMBIZWA MUHIMBILI

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    SIMBA SC imegawana pointi na mabingwa watetezi, Azam FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara jioni ya leo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam baada ya kufungana bao 1-1.
    Matokeo hayo, yanaifanya Azam FC ifikishe pointi 21 baada ya mechi 11, wakati Simba SC sasa inakuwa na pointi 13.
    Mshambuliaji wa Simba SC, Mganda Emmanuel Okwi aliifungia timu yake bao la kuongoza, kabla ya kuzimia kipindi cha pili kufuatia kugongana na beki Aggrey Morris wa Azam na kukimbizwa hospitali ya taifa, Muhimbili.
    Okwi alitibiwa kwa dakika 10 kwenye zahanati ndogo iliyopo ndani ya Uwanja wa Taifa, lakini hakupata nafuu akakimbizwa Muhimbili. 
    Emmanuel Okwi akiwa amebebwa kwenye machela kwenda kupakiwa kwenye ambulance akimbizwe hosptali
    Okwi alizimia akiwa tayari ameifungia Simba SC bao la kuongoza kipindi cha kwanza

    Mfungaji wa bao la Azam FC, Kipe Tchetche akimtoka kiungo wa Simba SC, Said Ndemla

    Mganda huyo, ambaye msimu uliopita alicheza kwa mahasimu, Yanga SC aliifungia Simba SC bao dakika ya 20 kwa shuti, baada ya kupokea krosi ya beki Hassan Ramadhani Kessy.
    Kessy alipoiga mpira mrefu kutoka kulia na ukap[itiliza hadi wingi nyingine alipokuwa Okwi, ambaye naye akatia majaro moja safi iliyoingia moja kwa moja nyavuni.
    Baada ya bao hilo, Azam FC walicharuka na kuanza kushambulia mfululizo ili kusawazisha, lakini wakaishia kukosa mabao ya wazi. 
    Dhamira ya Azam FC ilitimia mapema kipindi cha pili, walipofanikiwa kupata bao la kusawazisha dakika ya 57 kupitia kwa mshambuliaji kutoka Ivory Coast, Kipre Herman Tchetche.
    Halikuwa na tofauti sana na bao la Simba, kwani shambulizi lililozaa bao la Azam pia, lilitokana na mpira wa krosi uliotiwa na Khamis Mcha ‘Vialli’ aliyetoeka benchi kipindi cha pili.
    Azam FC ilichangamka zaidi baada ya kupata bao hilo na kuongeza kasi ya mashambulizi langoni mwa SImba SC, lakini wakaishia kukosa mabao ya wazi.
    Simba SC pia iliendelea kushambulia hata baada ya kusawazishiw abao, lakini nao waliishia kwenye kosa kosa.
    Kipindi cha pili mchezo ulitaka kuchafuka, baada ya wachezaji wa timu hizo kunaza kuchezeana rafu na wakati mwingine kulipiziana hata bila ya mpira.
    Refa wa mchezo huo, Kennedy Mapunda wa Mbeya aliyesaidiwa na Abdallah Selega na Hellen Mduma wote wa wa Dar es Salaam, aliwastaajabisha wengi kwa kushindwa kutoa kadi nyekundu hata moja, licha ya matukio kadhaa yaliyostahili adhabu hiyo.
    Kikosi cha Azam FC kilikuwa; Mwadini Ali, Shomary Kapombe, Erasto Nyoni, Aggrey Morris, Serge Wawa, Kipre Balou, Mudathir Yahya, Frank Domayo/Khamis Mcha, Didier Kavumbangu/Bocco, Kipre Tchetche/Kevin na Himid Mao.
    Simba SC; Peter Manyika, Kessy Ramadhan, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Isihaka Hassan, Juuko Murushid, Jonas Mkude, Ramadhani Singano ‘Messi’, Said Ndemla/Shaaban Kisiga, Dan Sserunkuma, Elias Maguri/Simon Sserunkuma na Emmanuel Okwi/Awadh Juma.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: OKWI AZIMIA BAADA YA KUIFUNGIA BAO SIMBA IKITOKA SARE NA AZAM, AKIMBIZWA MUHIMBILI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top