• HABARI MPYA

    Saturday, October 01, 2016

    MWISHO WA UBISHI LEO; NI SIMBA SC AU YANGA KUENDELEZA UBABE KWA MTANI?

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    BAADA ya tambo na majigambo ya muda mrefu, hatimaye imewadia siku ya kumaliza ubishi nani zaidi kati ya Simba na Yanga msimu huu.
    Miamba hiyo ya soka nchini, inakutana leo katika mchezo wa mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. 
    Na itakutana siku moja baada ya kurejea Jijini kutoka kwenye kambi zao za takriban wiki moja, Simba mkoani Morogoro na Yanga kisiwani Pemba.
    Ikiwa chini ya kocha mpya, Mcameroon Joseph Marius Omog, Simba inaongoza Ligi Kuu kwa pointi zake 16 baada ya mechi sita, ikishinda tano na sare moja, wakati Yanga iliyofungwa mchezo mmoja na sare moja na kushinda tatu, hivyo kuvuna pointi 10, ni ya tatu.   
    Vikosi vya Simba na Yanga vya msimu huu, leo vitaonyeshana kazi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam
    Simba wataingia uwanjani leo wakiwa na kumbukumbu ya kufungwa mechi zote za msimu uliopita, 2-0 kila moja; Septemba 26, mwaka 2015 mabao ya Amissi Tambwe dakika ya 44 na Malimi Busungu dakika ya 79 na Februari 20, mwaka 2016 mabao ya Donald Ngoma dakika ya  39 na Tambwe dakika ya 72.
    Mara ya mwisho Simba SC kuifunga Yanga ilikuwa ni Machi 8, mwaka 2015, bao pekee la Okwi dakika ya 52 katika mchezo wa marudiano wa Ligi Kuu, baada ya timu hizo kutoka sare ya 0-0 mechi ya kwanza 
    Oktoba 18, mwaka 2014.
    Kocha Mholanzi wa Yanga, Hans van der Pluijm anajivunia zaidi uzoefu wa kikosi chake kilichotwaa mataji yote matatu msimu uliopita, Ngao ya Jamii, Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), maarufu kama Kombe la Azam Sports Federation (ASFC) na Ligi Kuu.
    Uzoefu wa wachezaji kama Deo Munishi ‘Dida’, Ally Mustafa ‘Barthez’, Juma Abdul, Oscar Joshua, Mwinyi Mngwali, Kevin Yondan, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Mbuyu Twite, Vincent Bossou, Thabani Kamusoko, Simon Msuva, Haruna Niyonzima, Donald Ngoma na Amissi Tambwe ni jambo la kujivunia kabisa kwa kocha Pluijm kuelekea mchezo wa leo.
    Kwa pamoja na chipukizi kama Benno Kakolanya, Hassan Kessy, Pato Ngonyani, Andrew Vincent, Said Juma ‘Makapu’, Juma Mahadhi, Deus Kaseke, Geoffrey Mwashiuya, Malimi Busungu, Matheo Anthony na Abdallah Mguhi – Pluijm anayesaidiwa na Mzalendo, Juma Mwambusi anajikuta ana kikosi kipana na kizuri. 
    Omog, kocha wa zamani wa Azam FC, yeye ameisuka upya Simba baada ya kujiunga nayo Julai, akitengeneza mseto tishio wa wachezaji chipukizi na wakongwe wachache ambao atawajaribu kwa mara ya kwanza katilka mchezo dhidi ya mahasimu wa jadi, Yanga leo.
    Omog aliifunga timu yake ya zamani, Azam FC 1-0 akiwatumia Vincent Angban, Janvier Besala Bokungu, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Novaty Lufunga, Method Mwanjali, Shiza Kichuya, Muzamil Yassin, Laudit Mavugo aliyempisha Frederick Blagnon kipindi cha pili, Jonas Mkude, Ibrahim Hajib na Jamal Mnyate aliyempisha Said Ndemla dakika ya 63.
    Na katika mchezo wa leo hayatarajiwi mabadiliko makubwa sana, zaidi ya kiungo mkongwe Mwinyi Kazimoto na beki Mganda Juuko Murshid kuanzishwa labda.
    Bado Omog atakuwa na wachezaji wengine kama Peter Manyika, Hamad Juma, Malika Ndeule, Mohamed Ibrahim, Hajji Ugando na Ame Ali ambao yeyote kati yao anaweza kupewa nafasi na kufanuya vizuri. 
    Pamoja na kwamba, Mrundi Laudit Mavugo ametokea kuwa mfungaji wa mabao mengi ya timu hadi sasa, lakini Hajib anaweza kuwa tishio zaidi kwa safu ya ulinzi ya Yanga kutokana na kipaji chake na kujiamini, ukichanganya na uzoefu wa mechi za watani aliojikusanyia kwa misimu hii miwili.
    Japokuwa safu ya ulinzi ya Simba ina jemedari mpya, Mwanjali – lakini bado Ngoma na Tambwe wanatarajiwa kuendelea kuwa tishio leo.
    Tofauti ya Simba msimu uliopita na msimu huu ni kupatikana mchezaji mwenye kasi pembezoni mwa Uwanja, Kichuya ambaye dhahiri ameongeza kasi ya mashambulizi ya timu. 
    Lakini katika washambuliaji huwezi kubaini tofauti na labda wengine wanaona Hamisi Kiiza alikuwa hatari na bora zaidi ya Mavugo.
    Beki Hamad Juma aliyesajiliwa kutoka Coastal Union, alionekana kuwa mbadala sahihi wa Hassan Kessy aliyehamia Yanga, lakini baada ya kuanguka chooni na kulazimika kuwa nje hadi sasa, beki ya kulia imeonekana kidogo kupwaya.
    Kwa ujumla mchezo wa leo unatarajiwa kuwa mzuri, iwapo pia na uchezeshaji wa marefa, Martin Saanya, Samwel Mpenzu na Ferdinand Chacha nao utakuwa mzuri.
    Katika mchezo wa leo, kwa mara ya kwanza watazamaji wataingia kwa tiketi za Elektroniki ambazo zilianza kuuzwa tangu jana.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MWISHO WA UBISHI LEO; NI SIMBA SC AU YANGA KUENDELEZA UBABE KWA MTANI? Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top