• HABARI MPYA

    Monday, March 30, 2015

    MBWANA SAMATTA: TIMU LIGI KUU UFARANSA ILILIPA HADI FEDHA MAZEMBE, WAKAGOMA KUNIUZA, SIFURAHII MAISHA TENA LUBUMBASHI

    Na Mahmoud Zubeiry, MWANZA
    KLABU ya AS Saint-Etienne ya Ufaransa ilikwishaingiza fedha kwenye akaunti ya TP Mazembe ya DRC kumnunua mshambuliaji Mtanzania, Mbwana Ally Samatta, lakini mmiliki wa timu ya Lubumbashi, Moise Katumbi Chapwe akaitupia kapuni. 
    Hayo yamesemwa na Samatta mwenyewe katika mahojiano maalum na BIN ZUBEIRY mjini Mwanza jana na kwa sababu hiyo, mshambuliaji huyo wa zamani wa Simba SC, amesema hafurahii maisha tena Lubumbashi. 
    Samatta amesema baada ya kujiridhisha kwamba Moise Katumbi anambana kuondoka kwa kukataa ofa zote zinazoletwa, amejikuta hana furaha ile aliyokuwa nayo wakati anaingia Mazembe.
    Mbwana Samatta amesema hafurahii tena maisha Lubumbashi, baada ya klabu hiyo kukataa ofa za kumuuza Ulaya

    Akianza kuizungumzia ofa ya CSKA Moscow ya Urusi Desemba mwaka jana, Samatta anasema kwamba majeruhi na mizengwe vilichangia kupoteza nafasi hiyo. 
    Samatta aliumia katika wiki ya kwanza ya majaribio yake CSKA nchini Hispania, akalazimika kurejea Lubumbashi.
    “Kabla sijapata maumivu jamaa walionyesha kabisa nia ya kunisajili, wakauliza waongee na nani. Nikawapa mawasiliano ya wakala wangu, lakini tangu pale sikujua tena kilichoendelea,”.
    Samatta anasema na kwa bahati mbaya alipata maumivu wakati wa majaribio yake katika timu hiyo nchini Hispania, hivyo akashindwa kuendelea. “Baada ya kupata maumivu ndiyo ikawa sikuelewa tena kilichoendelea,”anasema Samatta ambaye Mkataba wake na TP Mazembe unamalizika Aprili mwaka 2016.
    Samatta anasema aliporejea Lubumbashi, alikutana na Moise Katumbi ambaye alimuambia kuna ofa ilikuja wakati akiwa Hispania kwenye mipango ya kujiunga na CSKA.
    “Hii ndiyo kawaida yake, ofa zinakuja lakini bosi hasemi, sijui kwa sababu ana mambo mengi au vipi. Na pale hakuna suala ambalo linaweza kuchukuliwa maamuzi bila yeye,”.
    “Yeye mwenyewe amekuwa akiniambia kuna ofa zilikuja, lakini hakukubaliana nazo kwa sababu mbalimbali. Lakini nabaki nashangaa, kwa nini anasema baada ya muda kupita,”anasema Samatta.
    Alipotakiwa kutaja baadhi ya ofa ambazo Katumbi alizikataa, Samatta anasema kwamba Standard Liege ya Ubelgiji walikuja kwa nia thabiti ya kutaka kumnunua, lakini mambo mawili kwa mujibu ya Katumbi yakakwamisha dili.
    Mbwana Samatta (kulia) akiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete (katikati) na Mtanzania mwenzake anayecheza naye TP Mazembe, Thomas Ulimwengu alipokutana nao mjini Kinshasa, DRC mwaka jana
    Samatta (kushoto) alipokuwa katika majaribio CSKA Moscow nchini Hispania

    “Kwanza alisema jamaa walitoa dau dogo sana, pamoja na sababu ya dau dogo, lakini bosi (Katumbi) akasema Standard Liege waliwahi kumfanyia uhuni wakati fulani,”. 
    “Aliwapelekea mchezaji mmoja Mkongo (Dieudonne ‘Dieumerci’ Mbokani Bezua) baada ya makubaliano ya bei, akenda Ubelgiji ili akafanyiwe vipimo vya afya. “Lakini katika vipimo kumbe walimpa kinywaji, ambacho wameweka dawa ambazo, alipokwenda kupimwa ikaonekana anatumia dawa za kulevya (zilizopigwa marufuku). Ikabidi dau la mchezaji lipungue,”anasimulia Mbwana.
    Anaendelea; “Lakini baadaye kuna mchezaji mwingine alikwenda akafanyiwa hivyo, ila wakala wake akashituka akaamua kusitisha biashara nao. Sasa wakala wa mchezaji anafahamiana na Katumbi, akamuambia. Kwa hvyo katumbi akarudisha kumbukumbu zake, akawachukia Standard Liege. Yaani kama wanatumia mbinu hizo kupata wachezaji kwa bei rahisi,”.
    Kwa sasa, Mbokani Bezua anachezea FC Dynamo Kyiv, baada ya awali kuchezea Anderlecht, VfL Wolfsburg, Monaco, Standard Liege na TP Mazembe.
    Samatta anasema ofa ya pili ilikuwa ya St Etienne ya Ufaransa, ambayo ilikuja wakati anakwenda Hispania kwenye majaribio na CSKA, Desemba mwaka jana.
    “Lakini bosi (Katumbi) alinificha akaja kuniambia baadaye, eti jamaa walituma hadi fedha katika akaunti ya Mazembe, baada ya kukwama kule dirisha la usajili likawa limefungwa nikarudi, ndiyo akaniambia jamaa walituma hadi fedha, ikabidi warudishiwe. Nikajiuliza kwa nini hakuniambia mapema. Nikaona analeta miyeyusho tu,”anasema kwa masikitiko Samatta.
    Mbwana Samatta kushoto akiichezea Taifa Stars dhidi ya Morocoo mwaka jana

    Kwa sababu zote hizo, Samatta anasema kwamba hafurahii maisha sana kwa sasa TP Mazembe, kama ilivyokuwa wakati anafika,”. Nahisi kama napoteza muda. Nafurahi kwa sababu nina marafiki, nafahamika, watu wananipenda. Sifurahii kubaki,”.
    “Ilikuwa nafasi nzuri ya mimi kuondoka ili nikakabiliane na changamoto nyingine, kwa sababu changamoto za hapa DRC nimekwishazimudu sana. Hapa Kongo ni kama nimemaliza. Nahitaji kusogea mbele, nikakutane na changamoto mpya ili nikuze uwezo wangu,”anasema.
    Pamoja na hayo, Samatta anasema kwamba Katumbi ameahidi dirisha kubwa atapokea ofa na amemkabidhi kwa wakala wake maalum ili wafanye naye kazi ya kusaka timu Ulaya.
    “Naamini sasa hivi hana ujanja, kwa sababu Aprili namaliza Mkataba wangu, hivyo ninaweza kuondoka bure, kwa hiyo atapokea fedha. Nina matumaini ya kuondoka mwishoni mwa msimu,”amesema.
    Mbwana Samatta enzi zake akiichezea Simba SC

    MBWANA ALLY SAMATTA ALIPOTOKEA…
    Mtoto wa Ally Samatta alizaliwa Januari 7, mwaka 1992 mjini Dar es Salaam na kisoka aliibukia katika timu ya Mbagala Market ya kwao, ambayo baadaye ilibadilishwa jina na kuwa African Lyon, baada ya kuchukuliwa na mmiliki mpya.  
    Alicheza African Lyon misimu miwili, 2008 hadi akahamia Simba SC, ambayo ndiyo ilimuuza TP Mazembe ambako hadi sasa amekwishacheza mechi 95 na kufunga mabao 60.
    Tanzania alianza kuchezea timu ya vijana chini ya umri wa miaka 20, baadaye akapandishwa timu ya wakubwa mwaka 2011, ambako hadi sasa katika mechi 20, ameifungia mabao 11.
    Bao la 11 alifunga jana katika sare ya 1-1 mchezo wa kirafiki wa kimataifa na Malawi Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza. Huyo ndiye Samatta na hayo ndiyo masahibu yake Lubumbashi, kiasi kwamba hafurahii tena maisha huko.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MBWANA SAMATTA: TIMU LIGI KUU UFARANSA ILILIPA HADI FEDHA MAZEMBE, WAKAGOMA KUNIUZA, SIFURAHII MAISHA TENA LUBUMBASHI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top