• HABARI MPYA

    Sunday, March 22, 2015

    AMISI JOSELYN TAMBWE: MKALI KWELI WA MABAO AMBAYE SIMBA ‘ILIBUGI’ KUMUACHA

    Na Mahmoud Zubeiry, TANGA
    KATIKATI ya wiki Simba SC ilifungwa mabao 2-0 na Mgambo Shooting Uwanja wa Mkwakwani, Tanga katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Matokeo hayo yamezidi kuiondoa Simba katika mbio za ubingwa- kutokana na kuachwa mbali na vinara, Yanga SC na mabingwa watetezi, Azam FC.
    Simba SC ambayo leo inacheza na Ruvu Shooting katika mchezo mwingine wa Ligi Kuu, Uwanja wa Mkwakwani, Tanga ina pointi 29 baada ya kucheza mechi 19, wakati Azam FC inayomenyana na Coastal Union Uwanja wa Mkwakwani leo, ina pointi 33 za mechi 17, huku Yanga SC wapo kileleni kwa pointi zao 37 za mechi 18.
    Yanga SC imefikisha pointi 37 baada ya ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Mgambo Shooting Uwanja wa Mkwakwani, Tanga jana- mabao ya Simon Msuva na Amisi Tambwe.
    Amisi Tambwe baada ya kuifungia bao la pili Yanga SC jana dhidi ya Mgambo Shooting-PAXP-deijE.gif

    Tambwe jana amefunga bao lake la saba katika mechi 16 tangu atue Yanga SC Desemba akitokea kwa mahasimu Simba SC, iliyomsajili msimu uliopita kutoka Vital’O ya Burundi.
    Simba SC ilimsajili Tambwe baada ya kuvutiwa naye kwa kuwa mfungaji bora wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati mwaka juzi nchini Sudan, akiiwezesha na Vita’O kutwaa taji la kwanza la michuano hiyo maarufu kama Kombe la Kagame.
    Simba SC ikanufaika na mabao ya Tambwe katika msimu uliopita wa Ligi Kuu akiibuka pia mfungaji bora wa Ligi Kuu.
    Ajabu, baada ya msimu ambao Tambwe alikuwa mfungaji bora wa klabu na Ligi Kuu, tetesi zilianza kwamba mchezaji huyo ataachwa kwa sababu hajui kupiga chenga.
    Tetesi zikazimwa na Tambwe akaichezea Simba SC mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu, lakini baada ya hapo, akaachwa katika dirisha dogo. Yanga SC ikajiokotea ‘dhahabu mchangani’ na sasa mchezaji huyo anawasaidia.
    Mwenyekiti wa Kamati ys Usajili, Zacharia Hans Poppe (kushoto) akiwa na Tambwe wakati anamsajili kutoka Vital'O mwaka juzi
    Amisi Tambwe enzi zake za utawala Simba SC. Lakini aliachwa kwa sababu hajui eti hajui kupiga chenga
    Mfumo wa Yanga SC wachezaji wote wa mbele wanafunga na Tambwe anafanya vizuri, anafunga na kuwatengenezea wenzake nafasi za kufunga. Wanamfurahia.
    Jana kawafungia bao Tanga, akitokea kufunga pia katika ushindi wa 2-1 dhidi ya Kagera Sugar. Kuwa mfungaji bora msimu huu tena ni vigumu, Mrundi mwenzake, Didier Kavumbangu wa Azam FC ambaye misimu miwili iliyopita alikuwa Yanga, yuko katika nafasi nzuri ya kurithi kiatu cha dhahabu.     
    Ukweli ni kwamba Simba SC imepoeteza mchezaji mzuri, mfungaji wa mabao asilia. Amisi Joselyn Tambwe aliyewafungia jumla ya mabao 26 katika mechi 43 ambaye sasa amehamishia makali yake Jangwani.
    Hata wasitamke hadharani, lakini ukweli ni kwamba wana Msimbazi hivi sasa wanajuta kumuacha Tambwe.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AMISI JOSELYN TAMBWE: MKALI KWELI WA MABAO AMBAYE SIMBA ‘ILIBUGI’ KUMUACHA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top