• HABARI MPYA

    Wednesday, September 25, 2013

    MAMLAKA MWANZA ZAAHIDI NYASI BANDIA NYAMAGANA

    Na Boniface Wambura, IMEWEKWA SEPTEMBA 25, 2013 SAA 10:47 JIONI 
    MAMLAKA za Mkoa wa Mwanza zimesema zitatimiza ahadi yao ya kuchangia dola 118,000 za Marekani (zaidi ya sh. milioni 190) ili kukamilisha mradi wa kuweka nyasi bandia kwenye Uwanja wa Nyamagana, jijini Mwanza kabla ya Oktoba 15 mwaka huu.
    Mkuu wa Mkoa (RC) wa Mwanza, Mhandisi Evarist Ndikilo pamoja na Mstahiki Meya wa Jiji la Mwanza, Stanslaus Mabula wametoa ahadi hiyo wakati wa kikao kati yao na Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga kilichofanyika leo (Septemba 25 mwaka huu) kwenye ofisi za TFF.
    Rais wa TFF, Leodegar Tenga (wa pili kushoto) akiwa na ujumbe wa Mkoa wa Mwanza ulioongozwa na Mkuu wa Mkoa, Mhandisi Evarist Ndikilo ulipomtembelea katika ofisi za TFF jana. Wa tatu kutoka kushoto ni Mstahiki Meya wa Jiji la Mwanza, Stanslaus Mabula akifuatiwa na Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza, Hida Hassan.

    Wakuu hao wa Mwanza katika kikao hicho pia walifuatana na Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza, Hida Hassan.
    TFF ilipeleka mradi wa Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) wa Goal Project IV wa nyasi bandia wa dola 500,000 za Marekani katika Uwanja wa Nyamagana.
    Mradi huo ulipelekwa huko baada ya Mkoa wa Mwanza kuahidi kuchangia dola 118,000 ili kukamilisha thamani ya mradi mzima ambayo ni dola 618,000 za Marekani. Wamiliki wa uwanja huo ni Jiji la Mwanza.
    Goal Project I ilitumika kwa ajili ya ujenzi wa hosteli ya TFF (technical centre), Goal Project II nyasi bandia Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume wakati Goal Project III iliweka nyasi bandia katika Uwanja wa Gombani ulioko Pemba, Zanzibar.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: MAMLAKA MWANZA ZAAHIDI NYASI BANDIA NYAMAGANA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top