• HABARI MPYA

    Sunday, October 07, 2012

    AL AHLY YANUSA FAINALI AFRIKA, AKINA SAMATTA WANA KAZI NA WENYE KOMBE LAO LEO

    Samatta ataiongoza Mazembe dhidi ya wenye Kombe leo Lubumbashi

    Na Prince Akbar
    MABINGWA mara sita Afrika, Al Ahly ya Misri wamelazimishwa sare ya kufungana mabao 3-3 na Sunshine Stars ya Nigeria katika mechi ya kwanza ya Nusu Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika jana iliyopigwa huko Ijebu-Ode kwenye Uwanja wa kimataifa wa Dipo Dina.
    Nahodha wa Sunshine, Godfrey Oboabona aliikosa mechi hiyo baada ya kuonyeshwa kadi ya pili ya njano katika mechi ya mwisho ya makundi dhidi ya Esperance ya Tunisia, wakati Mohamed Aboutrika anatumikia adhabu ya kufungiwa miezi miwili na Ahly.
    Ahly ilipata bao la kwanza dakika ya 18 kupitia kwa Mohamed Nagy, aliyefumua shuti kutoka nje ya boksi na kumtungua Moses Ocheje, kabla ya Mahdy El Sayed kuifungia bao la pili timu hiyo dakika ya 30, wakati Sunshine ilipata bao la kwanza dakika ya 40, kupitia kwa kiungo Mcameroon, Tamen Medrano aliyemtungua kwa shuti la mbali kipa wa Ahly, Sherif Elkramy.
    Wenyeji walisawazisha dakika ya 73 kwa mkwaju wa penalti wa Dele Olorundare baada ya Ajani Ibrahim kuangushwa kwenye eneo la hatari na Mohamed Nagy.
    Pamoja na hayo, Mashetani Wekundu wa Cairo walipata bao lililoelekea kuwa la ushindi, dakika moja badaaye kupitia kwa kijana mwenye umri wa miaka 25, Nagy ambalo lilikuwa bao lake la pili kwenye mechi hiyo.
    Beki wa Sunshine, Precious Osasco aliisawazishia timu yake dakika ya 83 kwa shuti la mpira wa adhabu lililomshinda kipa Elkramy.  Nagy alipata nafasi ya kukamilisha hat-trick dakika tatu kabla ya filimbi ya mwisho, lakini kichwa chake kiliupaisha mpira alipokuwa anaunganisha kona.
    Mechi ya marudiano itachezwa wiki ijayo Cairo katika Uwanja ambao mashabiki hawataingia na mshindi wa jumla atamenyana na mshindi kati ya mabingwa watetezi, Esperance na TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
    Ikiongozwa na washambuliaji wawili chipukizi wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta na Thomas Ulimwengu, leo Mazembe itaikaribisha Esperance mjini Lubumbashi katika Nusu ya Fainali ya pili.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AL AHLY YANUSA FAINALI AFRIKA, AKINA SAMATTA WANA KAZI NA WENYE KOMBE LAO LEO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top