• HABARI MPYA

    Sunday, October 07, 2012

    SIMBA SC KUZIDI KUPAA LIGI KUU LEO? INAMENYANA NA OLJORO JKT TAIFA

    Simba SC

    Na Prince Akbar
    LIGI Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, inataraiwa kuendelea leo kwa mabingwa watetezi na vinara wa ligi hiyo, Simba kuumana na Oljoro JKT kwenye  Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, mchezo ambao unatarajiwa kuwa mkali na wa kusimua.
    Katika mchezo huo, Simba SC itawakosa wachezaji wake wanne, wakiwemo beki Shomary Kapombe aliyeumizwa na mshambuliaji Said Bahanuzi wa Yanga Jumatano na Mrisho Ngassa, ambaye ana Malaria.  
    Ofisa Habari wa Simba SC, Ezekiel Kamwaga alisema jana katika Mkutano na Waandishi wa Habari, makao makuu ya klabu hiyo Mtaa wa Msimbazi kwamba, mbali na nyota hao wawili, wengine watakaokosekana kwenye mechi ya leo ni mabeki Amir Maftahi anayetumikia adhabu ya kadi na Haruna Shamte, ambaye pia ni majeruhi.
    Kamwaga alisema kwamba Kapombe aliumizwa na mshambuliaji wa Yanga, Said Bahanuzi Jumatano katika mechi baina ya watani hao wa jadi wa soka ya Tanzania, iliyopigwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kumalizika kwa sare ya 1-1.
    Kuhusu Ngassa, Kamwaga alisema kwamba baada ya mechi hiyo ya Jumatano, naye amepata Malaria, ambayo itamuweka nje ya Uwanja kesho, wakati Haruna aliumia mazoezini, timu hiyo ilipokuwa kambini Zanzibar ikijiandaa na mechi ya Yanga.
    Lakini Kamwaga alisema pamoja na kuwakosa nyota hao, anaamini wachezaji wengine watakaochukua nafasi zao watafanya vizuri. Kumbuka Emmanuel Okwi amemaliza adhabu na kesho anaweza kuiongoza Simba kwenye mechi hiyo. 
    Mechi ningine za leo ni kati ya vibonde wa ligi hiyo, Mgambo Shooting watakuwa wenyeji wa vibonde wengine wa ligi hiyo, Polisi Morogoro kwenye Uwanja wa Mkwakwani mjini Tanga, wakati Toto Africans wataikaribisha JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Kirumba mjini Mwanza na Tanzania Prisons watakuwa wenyeji wa Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya.
    Kagera Sugar wataikaribisha Yanga kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba kesho. Hadi sasa, mwenendo wa ligi unaonyesha ushindani ni kati ya mabingwa watetezi, Simba SC na washindi wa pili wa msimu uliopita, Azam FC ambazo zinakabana kileleni.
    Hali bado si nzuri kwa mabingwa wa kihistoria wa ligi hiyo, Yanga SC ambayo inazidiwa pointi tano na mabingwa watetezi, Simba SC ambao pia ni wapinzani wao wa jadi.
    Timu mbili kati ya tatu zilizopanda Ligi Kuu msimu huu JKT Mgambo na Polisi Morogoro ndizo zipo mkiani, wakati Prisons ndio inaonekana kuwa imara zaidi, kwani ipo nafasi ya tano katika msimamo huo.
    Katika mechi za jana, Azam FC iliisogelea zaidi Simba kileleni mwa Ligi Kuu baada ya kuifunga African Lyon bao 1-0 kwenye Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam.
    Azam ambayo ilimaliza mechi hiyo ikiwa pungufu ya mchezaji mmoja, baada ya beki wake, Samir Hajji Nuhu kutolewa nje kwa kadi nyekundu dakika ya 83 kwa kuonyeshwa kadi ya pili ya njano, imefikisha pointi 13 sawa mabingwa watetezi Simba, ambao wapo kileleni sasa kwa wastani wa mabao tu.
    Hadi mapumziko, Azam walikuwa tayari mbele kwa bao hilo, lililotiwa kimiani na mfungaji bora wa Ligi Kuu, John Raphael Bocco ‘Adebayor’ katika dakika ya kwanza ya muda wa nyongeza baada ya kutimu dakika 45 za kipindi cha kwanza.
    Hilo linakuwa bao lake la pili Adebayor msimu huu ndani ya mechi tano za Ligi Kuu, hali ambayo inaashiria kasi yake yake si ya kuridhisha msimu huu.
    Kikosi cha Azam kilikuwa; Mwadini Ally, Erasto Nyoni, Samir Hajji Nuhu, Aggrey Morris, Said Mourad, Ibrahim Mwaipopo/Salum Abubakar dk57, Jabir Aziz, Himid Mao/Abdulhalim Humud dk60, John Bocco ‘Adebayor’m, Kipre Tcheche na Abdi Kassim ‘Babbi’. 
    Katika mchezo mwingine jana, wenyeji Ruvu Shooting wameifunga Coastal Union ya Tanga mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Mabatini ulioko Mlandizi mkoani Pwani, mabao yaliyotiwa kimiani na Hussein Sued dakika ya sita na Hassan Dilunga dakika ya 12. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC KUZIDI KUPAA LIGI KUU LEO? INAMENYANA NA OLJORO JKT TAIFA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top