• HABARI MPYA

    Wednesday, November 03, 2021

    KAGERE ATOKEA BENCHI KUIPA USHINDI SIMBA


    MABINGWA watetezi, Simba wameilaza Namungo FC 1-0 usiku huu katika mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara Uwanja wa Benjamin Mkapa Jijini Dar es Salaam.

    Kagere aliyeingia dakika ya 72 kuchukua nafasi ya Nahodha, John Raphael Bocco, alifunga bao hilo akimalizia pasi ya beki wa kushoto, Mohammed Hussein‘Tshabalala’.
    Namungo FC ilimaliza pungufu baada ya kiungo wake Mzanzibari, Abdul Aziz Makame kutolewa kwa kadi nyekundu dakika ya 42 kwa kumchezea rafu Shomari Kapombe.
    Simba inafikisha pointi 11 na kupanda nafasi ya pili ikiwa inazidiwa pointi nne na vinara, Yanga SC baada ya wote kucheza mechi tano, wakati Namungo FC inabaki na pointi zake tano za mechi tano pia.
    Mechi nyingine za Ligi Kuu leo, Coastal Union imelazimishwa sare ya 0-0 na Tanzania Prisons Uwanja wa Mkwakwani Jijini Tanga kama ilivyokuwa kwa Biashara United na Mbeya City Uwanja wa Karume, Musoma mkoani Mara.
    Biashara sasa ina pointi sita, Coastal pointi nne, Mbeya City pointi saba na Prisons pointi mbili baada ya wote kucheza mechi tano pia.
    Pongezi kwa mfungaji wa bao hilo pekee mshambuliaji Mnyarwanda mwenye asili ya Uganda, Meddie Kagere dakika ya nne ya muda wa nyongeza baada ya kutimia dakika 90 za kawaida.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KAGERE ATOKEA BENCHI KUIPA USHINDI SIMBA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top