• HABARI MPYA

    Tuesday, August 27, 2019

    AZAM FC YAANZA VYEMA LIGI KUU TANZANIA BARA, YAICHAPA KMC 1-0 LEO UWANJA WA UHURU

    Na Saada Salim, DAR ES SALAAM
    TIMU ya Azam FC imeuanza vyema msimu mpya wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara baada ya ushindi wa 1-0 dhidi ya KMC Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam jioni ya leo.
    Pongezi kwa mshambuliaji mpya, Iddi Suleiman ‘Nado’ aliyesajiliwa kutoka Mbeya City aliyefunga bao hilo pekee dakika ya 14 tu ya mchezo akimalizia pasi ya beki Mganda, Nicolas Wadada kutoka upande wa kulia.
    Azam FC inayofundishwa na kocha wa KMC msimu uliopita, Mrundi Etienne Ndayiragijje ingeweza kuvuna mabao zaidi kama ingetumia vyema nafasi zake ilizotengeneza. 
    Iddi Suleiman ‘Nado’ameifunga bao pekee Azam FC ikiilaza KMC 1-0 leo Uwanja wa Uhuru 

    KMC ya kocha Mganda, Jackson Mayanja nayo haikuwa doro kabisa, kwani kupitia washambuliaji wake, Vitalis Mayanga, George Sangija na Hassan Kabunda ililitia majaribu lango la Azam FC mara kadhaa, lakini leo kipa Mghana, Razack Abalora alikuwa makini.
    Refa Isihaka Mwalile alimuonya kwa kadi ya njano kipa wa Azam FC, Razack Abalola dakika ya 85 kwa kosa la kuchelewa kupiga mpira.
    Ligi Kuu itaendelea kesho kwa mabingwa wa kihistoria, Yanga SC kumenyana na Ruvu Shooting ya Pwani kabla ya watetezi wa taji, Simba SC kupambana na JKT Tanzania, mechi zote zikipigwa Uwanja wa Uhuru mjini Dar es Salaam.
    Kikosi cha KMC kilikuwa; Jonathan Nahimana, Boniphace Maganga/Rayman Mgungila dk65, Ally Ramadhani/Amos Charles dk6, Abdallah Mfuko, Yussuf Ndikumana, Melly Sivirwa, Kelvin Kijili, Kenny Ally, Vitalis Mayanga, George Sangija/Hassan Kabunda dk53 na Serge Alain.
    Azam FC; Razack Abalora, Nicolas Wadada, Bruce Kangwa, Yakubu Mohammed, Daniel Amoah, Frank Domayo, Emmanuel Mvuyekure, Salum Abubakar ‘Sure Boy’/Abdallah Masoud ‘Cabaye’ dk67, Richard Ella D’jodi/Iddi Kipangwile dk55, Obrey Chirwa/Donald Ngoma dk67 na Idd Suleiman ‘Nado’.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: AZAM FC YAANZA VYEMA LIGI KUU TANZANIA BARA, YAICHAPA KMC 1-0 LEO UWANJA WA UHURU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top