• HABARI MPYA

    Wednesday, November 16, 2016

    MALINZI AMSHUKURU MEYA WA SEONGNAM KWA UKARIMU WALIOFANYIWA SERENGETI BOYS

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    RAIS wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi jana Novemba 15, 2016 alimtembelea Mstahiki Meya wa Jiji la Seongnam, Jae-myung Lee kumshukuru kwa namna ambavyo ameipokea timu ya taifa ya vijana wenye umri wa chini ya miaka 17 maarufu kwa jina la Serengeti Boys.
    Serengeti Boys walioko Korea kwa michezo ya kirafiki ya kimataifa ambako Jiji la Seongnam ni mshirika wa klabu ya Seongnam FC ambao ndio wenyeji wa timu yetu ya vijana ambayo ilifanya michezo miwili ya kirafiki ya kimataifa.
    Katika mazungumzo kocha huyo, Meya Jae-myung Lee aliiakikishia TFF kuwa jiji lake litaendelea kushirikiana na shirikisho katika kuendeleza mpira wa vijana wakike na wakiume.
    Jamal Malinzi amemtembelea Meya wa Seongnam, Jae-myung Lee kumshukuru kwa kuipokea Serengeti Boys

    Katika kumtembelea Meya huyo, Rais Malinzi aliambatana na Mkurugenzi wa Ufundi, Salum Madadi na benchi nzima la ufundi, linaloongozwa na Kocha Bakari Nyundo Shime na msaidizi wake, Muharami Mohammed Sultan pamoja na Mshauri Mkuu wa Maendeleo ya soka la vijana, Kim Poulsen.
    Baadaye jioni ya Novemba 15, 2016 Rais Malinzi alikutana na Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu la Korea Kusini (KFA), Chung Mong-Gyu ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Hyundai.
    Rais wa KFA Mong-Gyu naye alihakikishia TFF kuwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Korea litasaidia kuendeleza soka la vijana Tanzania sambamba na kusaidia mafunzo ya makocha.
    Wakati huo huo: TFF imepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za kifo cha Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Kagera (KRFA), Msafiri Ramadhani Msafiri.
    Taarifa za kifo hicho kilichotokea usiku wa kuamkia Novemba 15, mwaka huu akiwa njiani kwenda Hospitali ya Milagwe, Kampala nchini Uganda, imetolewa na Katibu Mkuu wa KRFA, Saloum Chama ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Utendaji TFF.
    Msiba huo umegusa familia ya mpira wa miguu akiwamo Rais wa TFF, Jamal Malinzi aliyemwelezea marehemu Msafiri alikuwa ni kiongozi mahiri na mwenye msimamo katika uamuzi wake.
    “Ni msiba mwingine mzito kwenye tasnia ya habari,” amesema Malinzi na kuongeza kuwa weledi wake katika uongozi utabaki kuwa alama kwa sisi tulio hai na kutakiwa kuenzi.
    Katika salamu zake za rambirambi, Malinzi ametuma kwa familia nzima ya mpira wa miguu Mkoa wa Kagera, familia, ndugu na jamaa huku akiwataka kuwa watulivu wakati huu mgumu wa kuomboleza kifo cha Msafiri anayetarajiwa kuzikwa leo kwenye makaburi ya Manispaa ya Kagera.
    Enzi zake, marehemu Msafiri kabla ya kuingia kwenye uongozi, alipata kuchezea Kurugenzi ya Bukoba, Balimi pia ya Bukoba mkoani Kagera ambako pia alichezea timu ya Mkoa katika mashindano ya taifa.
    Mbali ya kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi, Msafiri pia aliwahi kuwa Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu Karagwe kati ya mwaka 1999 hadi 2006.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MALINZI AMSHUKURU MEYA WA SEONGNAM KWA UKARIMU WALIOFANYIWA SERENGETI BOYS Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top