• HABARI MPYA

    Sunday, November 20, 2016

    MATUMLA KUZIPIGA MFULULIZO NOVEMBA NA DESEMBA DAR

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    BONDIA wa ngumi za kulipwa Mohammed Matumla atakuwa na mapambano mawili ndani ya miezi hii miwili kuanzia Novemba 27.
    Mtoto huyo wa bingwa wa zamani wa dunia wa WBU uzito wa Light-Middle, Rashid Matumla atapanda ulingoni Novemba 27 kwenye ukumbi wa Musoma Bar, Dar es Salaam kupigana na Abdallah Zamba katika pambano lisilo la ubingwa uzito wa Bantam.
    Baada ya pambano hilo, Matumla atarudi ulingoni Desemba 25 kuzipiga na Deo Samuel katika pambano lingine lisilo la ubingwa Uwanja wa Ndani wa Taifa, Dar es Salaam.
    Mohammed Matumla atakuwa na mapambano mawili ndani ya miezi hii miwili kuanzia Novemba 27

    Akizungumzia maandalizi ya mapambano yake, Matumla mdogo alisema kwamba yanaendelea vizuri na anatarajia kufanya vizuri katika mechi zote mbili zijazo.
    “Ngumi ni ngumi, siwezi kumdharau bondia yeyote, mimi ninajiandaa kikamilifu kwa mapambano yote. Natakiwa nifanye vizuri katika pambano la kwanza ili kujihakikisha kupanda ulingoni tena Krisimasi,”alisema jana Matumla.
    Matumla hajashinda katika mapambano yake mawili yaliyopita, akishindwa kwa Knockout (KO) na mwenyeji wake, Sakaria Lukas Novemba 6, mwaka huu ukumbi wa Ramatex Factory, mjini Windhoek, Namibia akitoka kutoa sare na Cossmas Cheka Machi 27, mwaka huu Uwanja wa Ndani wa Taifa, Dar es Salaam.
    Mara ya mwisho Moudy Matumla kushinda ilikuwa ni Februari 27, mwaka huu alipomshinda Bakari Mohamed viwanja vya Leaders Club, Kinodoni, Dar es Salaam.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MATUMLA KUZIPIGA MFULULIZO NOVEMBA NA DESEMBA DAR Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top