• HABARI MPYA

    Monday, November 21, 2016

    CLINTON WA YANGA KUZIKWA TANGA JUMATANO, ATASAFIRISHWA KESHO

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MAMAKAMU Mwenyekiti wa zamani wa Yanga, Isaac Shekiondo ‘Clinton’ (pichani kushoto) aliyefariki dunia usiku wa kuamkia jana, Dar es Salaam atazikwa Jumatano Korogwe, Tanga.
    Taarifa ya familia ilisema jana kwamba, msiba wa marehemu aliyefariki dunia baada ya kuugua kwa muda kwa sasa upo nyumbani kwake, Ilala Mchikichini Kota.
    Taarifa hiyo imesema shughuli za kuuaga mwili wa marehemu zitafanyika nyumbani kwake, Mchikichini kabla ya kusafirishwa kesho na mazishi yatafanyika Jumatano Korogwe kwa Shemsi.
    Shekiondo alikuwa Makamu Mwenyekiti katika Kamati ya Muda ya Yanga chini ya Mwenyekiti, Tarimba Abbas ‘Thabo Mbeki’ na enzi zake anakumbukwa kutokana na ukarimu wake na uwajibikaji mzuri.
    Rais wa  Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi alisema amezipokea kwa masikitiko makubwa taarifa za msiba wa Shekiondo.
    “Kwa kweli nimezipokea kwa masikitiko makubwa taarifa za msiba wa Shekiondo. Namfahamu vizuri yule bwana, tumefanya naye kazi Yanga. Na tulikuwa naye kwenye mpira siku zote,”alisema Malinzi.  
    Rais wa zamani wa Yanga, Francis Kifukwe naye pia alisema amezipokea kwa masikitiko makubwa taarifa za msiba wa Shekiondo.
    “Kwa kweli ni msiba wetu sote wana Yanga. Shekiondo tulikuwa naye Yanga tena katika kipindi kigumu sana, lakini tulishirikiana vizuri kusukuma mbele gurudumu la timu. Mungu amuweke pema peponi,”alisema Kifukwe.  Bwana ametoa, bwana ametwaa. Mungu ampumzishe kwa amani marehemu Shekiondo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: CLINTON WA YANGA KUZIKWA TANGA JUMATANO, ATASAFIRISHWA KESHO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top