• HABARI MPYA

    Wednesday, March 20, 2013

    SERIKALI, TFF ZAMALIZANA 'KIKUBWA'

    Rais wa TFF, Leodegar Tenga akizungumza na Waandishi wa Habari mchana wa leo katika ofisi za TFF, zilizopo ndani ya Uwanja wa Karume, Ilala, Dar es Salaam leo. Kulia ni Mwenyekiti wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Dioniz Malinzi. 

    Na Boniface Wambura
    SERIKALI imekubali mchakato wa uchaguzi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) uendelee kwa sharti la kuhakikisha haki inatendeka kwa wagombea waliofika mbele ya Kamati ya Rufani ya Uchaguzi.
    Akizungumza na Waandishi wa Habari leo mchana, Rais wa TFF, Leodegar Tenga amesema uamuzi huo umefikiwa kwenye kikao kati ya uongozi wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo chini ya Waziri Dk. Fenella Mukangara, TFF na Baraza la Michezo la Taifa (BMT).
    Amesema baada ya maafikiano hayo, TFF italiandikia barua Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) ambalo ndilo lililosimamisha mchakato huo ili litume ujumbe wake kwa ajili ya kusikiliza malalamiko ya wagombea walioenguliwa.
    Mwenyekiti wa BMT, Dioniz Malinzi kulia akifafanua jambo katika mkutano huo. Kushoto ni Tenga.
    Rais Tenga ambaye ameishukuru Serikali kwa kuruhusu mchakato huo uendelee, pia ameahidi kuwa uchaguzi wa TFF utafanyika kabla ya Mei 25 mwaka huu kama walivyokubaliana na Serikali, na kuwa haki si tu itatendeka bali ionekane imetendeka.
    “Serikali imetuelekeza uchaguzi ufanyike kabla ya Mei 25. Tumewaambia kwetu huko ni mbali. FIFA wakija hata kesho wakituambia endeleeni sisi tuko tayari. Hesabu zetu ziko tayari, makabrasha yote yako tayari yanasubiri mkutano tu. Labda itakuwa kutoa muda tu kwa wajumbe walioko mbali waweze kujiandaa, maana wajumbe huwezi kuwaita ghafla,” amesema.
    Amesisitiza kuwa TFF ilishapanga tarehe ya uchaguzi, lakini ukasimamishwa na FIFA baada ya baadhi ya walioenguliwa kulalamika huko. Hivyo maneno kuwa TFF hawataki uchaguzi kwa sababu wanataka kuendelea kubaki madarakani haya maana hata kidogo.
    Hivyo amewataka wagombea wote waliofika kwenye Kamati ya Rufani ya Uchaguzi na wakaendelea kujiandaa vizuri, kwani FIFA watakapofika watawasikiliza wao na vyombo vilivyowaengua.
    Pia amesema TFF ina heshimu Serikali na itaendelea kufanya hivyo, lakini vilevile lazima iheshimu FIFA sababu iko kwenye mpira wa miguu, na FIFA ndiyo wasimamizi wa mchezo huo duniani.  
    Amewakumbusha wanachama wa TFF, hasa wajumbe wa Mkutano Mkuu kufahamu kuwa TFF ina katiba, lakini ni lazima pia wafahamu kwanini kuna FIFA.
    Rais Tenga amewahadharisha watu wanaopitapita mikoani kuomba saini za wajumbe ili kuita Mkutano Mkuu wa dharura wakati wanajua mkutano ulishaitishwa, lakini ukasimamishwa na FIFA. Jambo hilo kikatiba ni kosa.
    Wakati huo huo: Tenga ameipongeza klabu ya Azam kwa ushindi wa mabao 2-1 ilioupata timu yake katika mechi ya raundi ya kwanza ya michuano ya Kombe la Shirikisho.
    Mechi hiyo dhidi ya Barrack Young Controllers II ilichezwa jijini Monrovia, matokeo ambayo yanaweka Azam katika nafasi nzuri ya kusonga mbele baada ya mchezo wa marudiano utakaofanyika wikiendi ya Aprili 6 au 7 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
    Amesema Azam imefanya jambo kubwa, kwani kushinda ugenini hasa katika nchi za Afrika Magharibi si jambo dogo, hivyo Watanzania waendelee kuiunga mkono na anaitakia kila la kheri katika mashindano hayo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: SERIKALI, TFF ZAMALIZANA 'KIKUBWA' Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top