• HABARI MPYA

    Thursday, March 28, 2013

    YANGA SC KUMKOSA HARUNA NIYONZIMA JUMAMOSI DHIDI YA POLISI MOROGORO

    Haruna Niyonzima; Amenusa tu na kuondoka Yanga kurejea nyumbani kwa matatizo ya kifamilia

    Na Mahmoud Zubeiry
    HARUNA Niyonzima hatakuwepo katika kikosi cha Yanga kitakachomenyana na Polisi Morogoro Jumamosi Uwanja wa Jamhuri, Morogoro kutokana na kusumbuliwa na matatizo ya kifamilia.
    Ofisa Habari wa Yanga, Baraka Kizuguto ameiambia BIN ZUBEIRY leo kwamba, kiungo huyo wa kimataifa wa Rwanda aliwasili jana nchini akitokea kwao Rwanda alipokwenda kwa majukumu ya kitaifa, lakini ameondoka tena kurejea kwao.
    “Kaja hapa kuomba ruhusa, mwalimu kamruhusu nasikia anauguliwa na mwanawe,”alisema Kizuguto.
    Kizuguto alisema wachezaji wengine wote wa kigeni wa Yanga wapo na wanaondoka na wenzao mchana wa leo kwenda Morogoro tayari kwa mchezo huo wa keshokutwa.   
    Hao ni beki Mbuyu Twite raia wa Rwanda pia na washambuliaji Hamisi Kiiza kutoka Uganda na Didier kavumbangu wa Burundi.
    Aidha, kipa Said Mohamed ameumia mazoezini leo asubuhi naye hatakwenda Morogoro. Kwa sababu hiyo, kipa aliyepandishwa kutoka kikosi cha pili, Yanga B, Yussuf Abdul ndiye atakayekaa benchi Jumamosi akimsikilizia Ally Mustafa ‘Barthez’.  
    Wachezaji wengine ambao hawatakwenda Morogoro ni majeruhi Omega Seme, Salum Telela na Ladislaus Mbogo pamoja na chipukizi waliopandishwa kutoka B, Rehani Kibingu na George Banda.
    Yanga SC inaongoza Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kwa pointi zake 48, ikifuatiwa na Azam FC yenye pointi 40, Simba SC 34 sawa na Kagera Sugar.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: YANGA SC KUMKOSA HARUNA NIYONZIMA JUMAMOSI DHIDI YA POLISI MOROGORO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top