• HABARI MPYA

    Monday, May 15, 2017

    KILA LA HERI SERENGETI BOYS, MALI LAZIMA WAKAE LEO

    Na Mahmoud Zubeiry, LIBREVILLE
    TIMU ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys inatupa kete yake ya kwanza katika michuano ya Mataifa ya Afrika, itakapomenyana na mabingwa watetezi, Mali Uwanja wa l’Amitie Sino mjini Libreville, Gabon.
    Kocha Mkuu wa Serengeti Boys, Bakari Nyundo Shime ameiambia Bin Zubeiry Sports – Online leo mjini hapa kwamba baada ya maandalizi mazuri ya muda mrefu, sasa wako tayari kuwafurahisha Watanzania.
    Lakini Shime amesema wanakutana na timu nzuri, ambayo bingwa mtetezi wa mashindano haya, hivyo kabisa wanatarajia ushindani mkali.
    “Utakuwa mchezo mgumu, Mali ndiye bingwa mtetezi wa haya mashindano na pia tumewafuatilia kwa kweli ni timu nzuri sana. Ila tu niseme sisi tumejipanga vizuri,”amesema.
    Serengeti Boys ilitua Gabon mapema wiki iliyopita ikitokea Cameroon ambako ilikuwa kambi ya wiki moja na kucheza michezo miwili ya kujipima nguvu dhidi ya wenyeji, ikishinda moja 1-0 na kufungwa moja 1-0 pia.
    Na ikumbukwe Serengeti Boys ilikwenda Cameroon ikitokea mjini Rabat nchini Morocco ambako iliweka kambi ya mwezi mmoja kujiandaa na michauno inayotarajiwa kuanza Mei 14 hadi 28.
    Pamoja na kambi ya mazoezi, Serengeti Boys ikiwa mjini Rabat, Morocco ilicheza mechi mbili za kirafiki dhidi ya Gabon na kushinda 2-1 kila mchezo.
    Awali Serengeti Boys iliifunga Burundi mara mbili, Machi 30 mabao 3-0 na Aprili 1 mabao 2-0, mechi zote mbili zikipigwa Uwanja wa Kaitaba, Bukoba, kabla ya kulazimishwa sare ya 2-2 na Ghana ‘Black Starlets’ Aprili 3 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Michuano hiyo ilianza rasmi jana kwa wenyeji, Gabon kufungwa 5-1 na Guinea, wakati Ghana nayo iliilipua Cameroon 4-0.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KILA LA HERI SERENGETI BOYS, MALI LAZIMA WAKAE LEO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top