• HABARI MPYA

    Tuesday, February 14, 2017

    MAYANGA AWAKABIDHI TFF PROGRAMU YA TAIFA STARS

    Na Rehema Lucas, DAR ES SALAAM
    SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limepokea programu ya miezi sita ya timu ya taifa, Taifa Stars kutoka kwa kocha wa muda, Salum Mayanga, anayekaimu nafasi iliyoachwa wazi na Charles Boniface Mkwasa ambaye kwa sasa ni Katibu wa Yanga SC.
    Akizungumza na Waandishi wa Habari leo mjini Dar es Salaam, Ofisa Habari wa TFF, Alfred Lucas Mapunda amesema kwamba programu hiyo itahusisha kambi za mazoezi na michezo ya kirafiki.
    Mapunda amesema kwamba kwa ujumla Mayanga amewasilisha programu ya maandalizi ya kufuzu kwa Fainali za Michuano ya Ubingwa wa Mataifa ya Afrika (CHAN), inayohusisha wachezaji wanaocheza ligi za nchini mwao pekee na Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON). 
    TFF imekabidhiwa programu ya Taifa Stars ya maandalizi ya mechi za kufuzu AFCON na CHAN

    “Michezo ya kirafiki ni kocha Mayanga ndiye atapendekeza ichezwa nje ya nchi au ndani, lakini pia programu hiyo inaelezea juu ya maandalizi ya mechi ya CHAN ya 2018 na AFCON ya 2019 Cameroon,”amesema Lucas.
    Taifa Stars itaanza na Rwanda katika kuwania tiketi ya CHAN mwakani nchni Kenya na mechi ya kwanza itachezwa Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam kati ya Julai 14 na 16 kabla ya timu hizo kurudiana Uwanja wa Amahoro, Kigali kati ya Julai 21 na 23.
    Ikifanikiwa kuitoa Rwanda, Tanzania itamenyana na mshindi kati ya Uganda na ama Sudan Kusini au Somalia katika Raundi ya Tatu ya mchujo mechi ya kwanza ikichezwa kati ya Agosti 11, 12 na 13 na marudiano kati ya Agosti 18, 19 na 20, mwaka huu.
    Tanzania imewahi kushiriki mara moja tu fainali za CHAN, ambayo ilikuwa ni mwaka 2009 zikifanyika kwa mara ya kwanza kabia.
    Kwa upande wa AFCON, Taifa Stars imepangwa Kundi L pamoja na Uganda, Cape Verde na Lesotho.
    Mshindi wa kila kundi atafuzu moja kwa moja AFCON ya 2019, wakati timu nyingine tatu zitakazomaliza nafasi ya pili na wastani mzuri zaidi ya nyingine zitafuzu kama washindi wa pili bora. 
    Tanzania imewahi kucheza mara moja tu fainali za AFCON, mwaka 1980 nchini Nigeria ambako ilitolewa hatua ya makundi.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MAYANGA AWAKABIDHI TFF PROGRAMU YA TAIFA STARS Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top