• HABARI MPYA

    Thursday, February 16, 2017

    MANJI AACHIWA KWA DHAMANA BAADA YA KUSOMEWA SHITAKA LA KUTUMIA DAWA ZA KULEVYA

    Na Princess Asia, DAR ES SALAAM
    MWENYEKITI wa Yanga SC, Yussuf Manji ameachiwa kwa dhamana, baada ya kusomewa shitaka la tuhuma za kutumia dawa za kulevya mchana wa leo Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam.
    Baada ya kusoma shitaka hilo, Hakimu Cyprian Mseha alimtaka mtuhumiwa huyo kufika mahakamani hapo Machi 16 kwa mwendelezo wa kesi hiyo.
    Bahati nzuri dhamana iliyowekwa na Katibu wa Yanga, Charles Boniface Mkwasa kwa Sh. Milioni 10 ikakubaiwa na akaachiwa huru, akirejea nyumbani kwake tangu alipoondoka Alhamisi iliyopita.
    Manji aliwasili mahakamani chini ya ulinzi wa Polisi, akitokea kituo kikuu cha Polisi, Dar es Salaam alikuwa amewekwa rumande tangu Alhamisi.
    Mwenyekiti wa Yanga SC, Yussuf Manji akiingizwa kwenye chumba cha Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam kujibu mashitaka ya tuhuma za kutumia dawa za kulevya PICHA ZAIDI GONGA HAPA

    Hata hivyo, Jumamosi mchana Manji alipelekwa hospitali ya Taifa, Muhimbili, Dar es Salaam baada ya hali yake kubadilika na kuwa mbaya ikiwelezwa anasumbuliwa na matatizo ya moyo.
    Taarifa zilisema Manji alifanyiwa upasuaji mdogo na kurejeshwa Polisi jana, kabla ya leo kupandishwa mahakamani. 
    Manji aliwekwa rumande baada ya kujisalimisha mwenyewe kituo kikuu cha Polisi Alhamisi iliyopita, baada ya kutajwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda katika orodha ya watu 65 wanaoshukiwa kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya.
    Japokuwa Manji na wengine wote 64 waliotajwa walitakiwa kuripoti Polisi Ijumaa, lakini yeye alijipeleka mwenyewe Alhamisi pamoja na Askofu Gwajima, ambaye aliachiwa baada ya siku mbili.
    Na wakati tuhuma zake zikibadilika kutoka kwenye kushukiwa kuuza hadi kudaiwa anatumia dawa za kulevya, Manji pia anakabiliwa na shitaka lingine kupitia kampuni yake ya Quality Group Limited, kuajiri wageni bila vibali vya kufanya kazi nchini.
    Ofisa wa Idara ya Uhamiaji Dar es Salaam, John Msumule, alisema juzi kwamba Manji anatakiwa kufika ofisini hapo kujibu mashitaka ya kuajiri watu 25, ambao hawana vibali vya kufanya kazi nchini. 
    Msumule alisema ilikuwa wamkamate Manji Jumatatu wiki hii, lakini wakaambiwa amelazwa hospitali, hivyo wameacha maagizo akitoka hospitalini aripoti mwenyewe Ofisi ya Uhamiaji makao makuu Dar es Salaam.
    Msumule alisema kwamba walifanikiwa kukamata pasipoti 126 zenye makosa Jumamosi na kati ya hizo, 25 zilikuwa za waajiriwa ambao hawana vibali.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MANJI AACHIWA KWA DHAMANA BAADA YA KUSOMEWA SHITAKA LA KUTUMIA DAWA ZA KULEVYA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top