• HABARI MPYA

    Wednesday, May 27, 2015

    SIMBA SC YASAJILI MABEKI WA AZAM NA JKT RUVU

    Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
    SIMBA SC imesajili mabeki wawili wa Kizanzibari, Samir Hajji Nuhu wa kushoto na Mohammed Fakhi wa kati usiku wa leo.
    Nuhu alikuwa mchezaji wa Azam FC kwa misimu miwili hadi msimu wa 2013/2014 kabla ya kuumia goti na kuondolewa katika usajili, wakati Fakhi msimu huu amechezea JKT Ruvu.
    Mabeki hao vijana wadogo wamesaini leo mikataba ya kuitumikia Simba SC, Nuhu mwaka mmoja na Fakhi miaka miwili.
    Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe ameambia BIN ZUBEIRY usiku huu kwamba wanatarajiwa mambo mazuri kutoka kwa wachezaji hao vijana wadogo.
    Fakhi akisaini SImba SC leo mbele ya Mjumbe wa Kamati ya Utendaji, Collins Frisch 

    “Huyu Nuhu kwa wenye kumkumbuka alipokuwa Azam FC kabla ya kuumia. Na yeye ndiye aliyekuwa beki chaguo la kwanza upande wa kushoto. Lakini baada ya kupitia vipimo vyake na kujiridhisha kwamba amepona kabisa, tumempa nafasi nyingine,”amesema Poppe.
    Aidha, Kapteni huyo wa zamani wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), amesema Fakhi alikuwa beki tegemeo wa kati wa JKT Ruvu msimu huu na wengi walivutiwa na ukabaji wake mzuri.
    “Mimi binafasi niseme ni mmoja kati ya watu waliopendezewa na ukabaji wa huyu kijana. Lakini si hivyo, kama utakumbuka mechi yetu ya mwisho  ya Ligi tulicheza na JKT Ruvu, hivyo baada ya mechi hata benchi la Ufundi lilimpendekeza huyu mchezaji,”amesema.
    Wawili hao wanafanya idadi ya wachezaji wapya waliosajiliwa Simba SC kufika watatu baada ya mwanzoni mwa wiki kusajiliwa kiungo wa Mbeya City, Peter Mwalyanzi.
    Simba SC imekuwa na bahati ya kuwasajili wachezaji wote hao wote wakiwa huru baada ya kumaliza mikataba yao katika klabu zao. 
    Nuhu akisaini Mkataba wa Simba SC leo mbele ya Frisch
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIMBA SC YASAJILI MABEKI WA AZAM NA JKT RUVU Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top