• HABARI MPYA

    Saturday, May 23, 2015

    BOT MAKAO MAKUU ULIMI NJE KWA BOT ZENJI

    Na Samira Said, DAR ES SALAAM
    TIMU ya soka ya Benki Kuu Tanzania (BOT) makao makuu, leo imeshindwa kuwafunga wageni wao timu ya benki hiyo tawi la Zanzibar na kulazimishwa suluhu katika mchezo wa kirafiki uliofanyika leo asubuhi kwenye Uwanja wa Sigara, Chang'ombe jijini Dar es Salaam.
    Katika mchezo huo timu zote zilitengeneza mashambulizi mara kwa mara lakini washambuliaji wao hawakuwa makini katika umaliziaji na kufanya dakika 90 zimalizime kila upande ukikosa bao la kufutia machozi.
    Hata hivyo wenyeji timu ya Makao Makuu watajilaumu kwa kukosa ushindi baada ya mchezaji wake, Alex Makene kupaisha juu mpira wa penalti iliyotolewa na refa, Ephraim Suka baada ya mshambuliaji wa timu ya Zanzibar kumfanyia madhambi nyota wa makao makuu.


    Timu hizo zinatarajiwa kurudiana hivi karibuni Visiwani Zanzibar baada ya wenyeji kukamilisha taratibu za kuwapokea wenzao.
    Bonanza hilo lilifunguliwa na Naibu Mkurugenzi wa BOT, Juma Reli ambaye aliwaambia wachezaji wanatakiwa kutumia michezo kujenga urafiki, undugu, nidhamu na heshima.
    Reli alisema kuwa michezo inasaidia kujenga afya na inaongeza mahusiano mazuri kazini na kuwataka wafanyakazi hao wawe na tabia ya kufanya mazoezi mara kwa mara.
    Mratibu wa bonanza hilo, Ambonisye Mwasengo, alisema kuwa lengo na benki hiyo kuanzisha bonanza hilo ni kutaka kujenga karibu mahusiano ya wafanyakazi na makao makuu na kwenye matawi yao.
    Alisema kuwa kupitia mabonanza watakayokuwa wanafanya yatasaidia wafanyakazi wao kuwashawishi kupenda mazoezi ambayo yatawasaidia kuondoa msongo wa mawazo.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BOT MAKAO MAKUU ULIMI NJE KWA BOT ZENJI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top