• HABARI MPYA

    Friday, November 01, 2013

    KWAKO MALINZI, JE NAWE NI MUUMINI WA FEDHA KULIKO AMANI NA USALAMA?

    Na Mahmoud Zubeiry, Dar es Salaam
    KATIKA wiki moja, ndani ya siku nne yametokea matukio mawili ya vurugu zilizosabaisha watu kujeruhiwa na uharibifu wa mali katika viwanja vya soka nchini, wakati wa mechi za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Kiasi cha saa 24 tangu Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) lipate uongozi mpya chini ya Rais Jamal Emil Malinzi kufuatia uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 27, mwaka huu ukumbi wa NSSF Water Front, Dar es Salaam, mashabiki wa klabu inayocheza Ligi Kuu kwa mara ya kwanza, Mbeya City waliukaribisha uongozi huo mpya kwa staili ya aina yake.   
    Waliwafanyia fujo mashabiki wa Prisons katika mchezo baina ya timu hizo, Mbeya City ikishinda 2-0, ikiwemo kujeruhi na kuharibu mali, kwa kupiga mawe magari na kupasua vioo Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya. 
    Katika utawala uliomaliza muda wake TFF, chini Rais Leodegar Tenga (kushoto) vurugu vviwanjani zilikumbatiwa, je Rais mpya wa TFF Jamal Malinzi (kulia), utawala wake nao utalea hali hiyo?

    Kwa mashabiki wa Mbeya City, hilo linakuwa tukio la pili katika mzunguko huu wa kwanza pekee, baada ya awali kuwafanyia hivyo Yanga mwezi uliopita, ikiwa ni pamoja kupasua vioo vya basi la timu hiyo na kumjeruhi dereva wake katika mechi baina ya timu hizo pamoja na gari nyingine. 
    Na jana- Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam uligeuka eneo la vita baina ya Polisi mashabiki wa Simba SC, kufuatia Kagera Sugar kupata bao la kusawazisha dakika ya pili ya muda wa nyongeza baada ya kutimia kwa dakika 90 za mchezo timu hizo zikitoka 1-1.
    Baada ya Salum Kanoni kukwamisha nyavuni mkwaju wake wa penalti, mashabiki wa Simba waliokuwa viti vya Rangi ya Bluu na Chungwa, walianza kung’oa viti na kuvitupia uwanjani.
    Mara moja, Polisi walianza kupambana na mashabiki hao kwa kuwatupia mabomu ya machozi, ndipo wakaanza kukimbia. Makocha na wachezaji wa Simba kwa pamoja waliwafuata waamuzi kuwalalamikia- hali ambayo ilifanya watolewe kwa kusindikizwa na Polisi. Simba ilitangulia kufunga kupitia kwa Amisi Tambwe dakika ya 45.
    Kutokana na vurugu hizo mashabiki wengi walijeruhiwa na kupatiwa huduma katika Zahanati ndogo ya Uwanja wa Taifa na wengine kukimbizwa Hospitali ya Temeke, huku waliondoka na maumivu yao. Watu pia waliporwa simu, fedha na vitu mbalimbali vya thamani.
    Basi la Yanga lilipasuliwa vioo Mbeya

    Dereva akajeruhiwa namna hii, bahati nzuri haikuwa jichoni
    Miongoni mwa walioporwa ni mmiliki wa hoteli ya Sapphire Court, Abdulfatah Salim Saleh wakati anateremka jukwaani, akaibiwa simu yake aina ya Blackberry Q10, yenye thamani ya Sh. Milioni 1.8.
    “Tunateremka kukawa na tatizo na milango ya kutokea watu wengi mlango mdogo, milango mingine imefungwa, sasa pale watu wengi tu wameibiwa wengine walikuwa wanalia kuibiwa pochi za fedha zina dola,”alisema Abdulfatah.
    Tukio la jana kwa ujumla linakuwa la nne kubwa la vurugu katika msimu huu wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, baada ya awali mashabiki wa Yanga kushambulia basi la Coastal Union, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kujeruhi mmoja wa wachezaji wa timu hiyo.
    Baada ya vurugu za kwenye mchezo wa Yanga na Coastal na Union, Kamati ya Ligi Kuu ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) iliitoza Yanga faini ya Sh. Milioni 1, yaani Sh. 500,000 kwa kila kosa, kutokana na washabiki wake kuwarushia waamuzi chupa za maji baada ya Coastal Union kusawazisha bao katika mechi hiyo na kuwarushia chupa waamuzi hao wakati wakirejea vyumbani baada ya pambano hilo.
    Watu wa huduma ya kwanza sasa wana jukumu la kubeba na mashabiki waliojeruhiwa katika viwanja vyetu na si wachezaji pekee wanaoumia uwanjani kwa rafu za mchezo 

    Suala la kushambuliwa kwa basi la Coastal halikuchukuliwa hatua na sababu hazikuelezwa. 
    Ajabu kocha wa makipa wa Coastal Union, Juma Pondamali aliyewakejeli tu mashabiki Uwanja wa Taifa, alipewa adhabu kubwa kuliko Yanga SC, kwa kupigwa faini ya Sh. Milioni 1 na kufungiwa miezi mitatu.
    Marefa waliochezesha mechi hiyo, Martin Saanya na msaidizi wake namba moja, Jesse Erasmo nao wamefungiwa mwaka mmoja kila mmoja kwa kutoimudu mechi hiyo.
    Baada ya yaliyotokea katika mchezo wa Yanga na Coastal niliandika; Samaki mkunje angali mbichi na ni bora kuchukua tahadhari kabla ya hatari. TFF, imekuwa ikinyamazia matukio yenye dalili za kuleta athari kubwa zaidi mbele, jambo ambalo hakika si zuri.
    Haikuwa mara ya kwanza kwa mashabiki wa Yanga kufanya fujo uwanjani na kusababisha uharibifu wa mali na hata kujeruhi na kwa ujumla kuhatarisha amani. Wenye soka yao, FIFA wanauita mchezo wa kiungwana- hawataki uhuni hata kidogo na TFF kama wasimamizi wakuu wa soka nchini, wanapaswa kulizingatia hilo.
    Lakini tatizo kubwa, TFF wanashindwa kuchukua adhabu ambazo zitakuwa fundisho kwa mashabiki wa Yanga na wengine wote, kwa sababu wameweka mbele fedha kuliko utu na thamani ya mchezo wenyewe.
    Namna hii mtu anaweza kukanyagwa hadi kufa...Malinzi angalia hii

    Nilisema, wakati umefika sasa, Yanga ipewe adhabu ya kucheza mechi bila mashabiki uwanjani, japo mechi tatu tu na bila shaka baada ya kukosa fedha, viongozi wake wataona umuhimu wa kuwasihi mashabiki wao wawe wastaarabu. Lakini kama tutaendelea na ile desturi ya faini Sh. 500,000 na kutakiwa kufidia gharama za uharibifu na tiba za waliojeruhiwa, hakika iko siku litakuja kutokea kubwa.
    Nilisema, ni wazi kama tunataka kuivusha soka yetu katika hatua nyingine, lazima kwanza tukubali kujivua ushabiki na kuchukua hatua ambazo moja kwa moja zitalenga maslahi na ustawi wa mchezo huu nchini. Wakati umefika sasa, tuondoe dhana kwamba Simba na Yanga haziwezi kupewa adhabu kali, kisa ni timu kubwa na zinazalisha mapato mengi. Si sahihi.
    Inawezekana huyu hata hakufanya vurugu, ila kwa kuwa likuwepo katika eneo ambalo vurugu zilitokea na akachelewa kukimbia hadi Polisi wakamkamata, ndiyo anatolewa kafara. 

    Sasa matokeo yake na mashabiki wa mikoani nao wanaiga vurugu, tena wanazifanya kisawasawa na kuhatarisha amani kabisa. Bado najiuliza, kama mashabiki wa Yanga baada ya vurugu zote walizofanya dhidi ya Coastal, timu yao ingepewa adhabu ya kucheza bila mashabiki japo mechi moja tu, je na mashabiki wa Mbeya City jana wangefanya walichokifanya? 
    Mfano mdogo tu; wakati fulani mashabiki wa Ashanti walifanya vurugu katika mechi dhidi ya Yanga SC na wakafungiwa kucheza Uwanja wa Taifa na sasa timu yao imerejea Ligi Kuu wamekuwa na nidhamu ya hali ya juu, wakikumbuka adhabu waliyowahi kupata. 
    Sasa Mbeya City wamerudia tena na Simba SC jana wamefanya yao, kwa sababu hata tukio la kwanza wahusika hawakupewa adhabu ya kuwafanya waogope kufanya hivyo tena- maana yake tutarajie Manungu, Mkwakwani, Kaitaba, Mwinyi na Sheikh Amri Abeid nako iko siku ‘kitanuka’. Vema mwishoni mwa wiki soka ya Tanzania imepata viongozi wapya, chini ya Jamal Malinzi (Rais) na hizi zinakuwa changamoto za awali kwao.
    Waliohusika wenyewe jana walilala nyumbani na familia zao na leo wanaendelea na shughuli zao kama kawaida na mechi ijayo na Ashanti United watakuja tena Taifa

    Mwanzoni mwa utawale wake FIFA, Rais wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), Sepp Blatter aliwahi kusema; “Soka na vurugu ni chanda na pete”- kwa sababu anafahamu mashabiki wanaongozwa na hisia.
    Kutaka kusubiri Polisi wapambane na mashabiki ni kukaribisha upotevu wa amani katika viwanja vyetu vya soka na matokeo yake, watu wataogopa kwenda viwanjani na klabu zitaathirika kimapato.
    Lazima TFF izipe jukumu klabu kuwatuliza mashabiki wao, kwa kuchukua hatua kali ambazo zitasaidia hata mashabiki wenyewe kwa kusemezana, kuhamasishana utulivu uwanjani. Sitaki kuamini Malinzi na Kamati yake mpya ya Utendaji watakuwa waumini wa fedha kuliko amani na usalama katika mchezo wenyewe.
    Ukisema unawafungia Simba kwa sasa, utawaonea kwa sababu msimu huu Yanga na Mbeya City wamekwishafanya vurugu- iundwe kanuni hiyo katika kanuni zetu za michezo na itangazwe kwamba kuanzia mzunguko wa pili, vurugu zitaigharimu klabu kucheza bila mashabiki. Basi. Kwako Malinzi.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: KWAKO MALINZI, JE NAWE NI MUUMINI WA FEDHA KULIKO AMANI NA USALAMA? Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top