Said Bahanuzi |
Na Mahmoud Zubeiry
MSHAMBULIAJI wa Yanga, Said Bahanuzi ‘Spider Man’ anatarajiwa
kuanza mazoezi mepesi keshokutwa kufuatia kuchanika nyama za paja la mguu wa
kulia katika mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Kagera Sugar kwenye
Uwanja wa Kaitaba, Bukoba Jumatatu wiki hii.
Bahanuzi aliumia dakika ya 23, baada ya kugongana na beki
Benjamin Effe wa Kagera Sugar na kushindwa kuendelea na mchezo, nafasi yake
ikichukuliwa na Jerry Tegete katika mechi ambayo Yanga ililala 1-0, beo pekee
la Themi Felix.
Daktari wa Yanga, Sufiani Juma ameiambia BIN ZUBEIRY asubuhi ya
leo kwamba, mfungaji huyo bora wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe
la Kagame, anaendelea vizuri baada ya kuchanika nyama za paja la mguu wa kulia.
Yondan alivyoumizwa na Boban |
“Lini haswa ataingia kwenye programu kamili ya mazoezi,
itategemea na maendeleo yake atakapoanza mazoezi mepesi,”alisema Sufiani.
Kuhusu beki Kevin Yondan aliyeumia kwenye mechi dhidi ya
Simba SC, Oktoba 3, mwaka huu baada ya kugongwa na Haruna Moshi ‘Boban’,
Sufiani alisema naye anaendelea vizuri na wakati wowote wiki ijayo ataanza
mazoezi mepesi.
Zaidi ya hao, Sufiani alisema Yanga ina majeruhi mwingine
mmoja tu, ambaye ni Salum Telela ambaye naye anaendelea vizuri.
Bahanuzi ndiye tegemeo la mabao la Yanga kwa sasa, kwani tangu
ajiunge na timu hiyo akitokea Mtibwa Sugar msimu huu, ameifungia mabao 12 katika
mechi 13, ikiwemo ile dhidi ya Kagera aliyocheza kwa dakika 23 kabla ya kuumia
na kutoka.
Baada ya ushindi wa mabao 3-1 katika mechi ya Ligi Kuu mjini
Mwanza, Yanga inatarajiwa kuendelea na mazoezi Jumatatu, kujiandaa na mechi
ijayo, dhidi ya Ruvu Shooting Oktoba 20, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.