Hanspop |
KLABU ya Simba imesema itamfikisha mahakamani mchezaji Mbuyu
Twite wa klabu ya APR kwa kosa la kuwatapeli na kukubali kusajiliwa na Yanga.
Mwenyekiti wa kamati ya Usajili ya Simba, Zakaria Hanspope amekaririwa
na liwazozito.blogspot.com akisema,
Twite alishapokea fedha za Simba na kukubali kuingia nayo mkataba, hivyo hawezi
kwenda kinyume.
Hanspope alisema kilichofanywa na Yanga kumshawishi mchezaji
huyo arejeshe fedha za Simba na kupokea fedha zao ni cha kihuni na hawawezi
kukivumilia.
Alisema kama ni kurejesha fedha zao, anayepaswa kufanya
hivyo ni Twite mwenyewe na si klabu ya Yanga.
Hanspope alisema wao waliingia mkataba na Twite kupitia klabu
yake ya APR na Shirikisho la Soka la Rwanda, hivyo walipaswa kuomba hati ya
uhamisho kutoka Rwanda na si Congo.
"Haya mambo lazima ufike wakati yafikie mwisho.
Haiwezekani klabu imesikia kwamba mchezaji amesajiliwa na klabu fulani na
yenyewe inamfuata kuzungumza naye,"alisema.
Hanspope alisema bado wanaamini kwamba Twite ni mchezaji wao
na kama itatokea vinginevyo, watapambana hadi haki yao ipatikane.
Yanga imemsajili Twite, wakati tayari akiwa amekwishaini
Simba SC, baada ya kumrudisha kwenye uraia wake wa asili, Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Kongo (DRC), badala ya Rwanda aliopewa wakati akicheza nchini
humo na kumbadili jina pia.
Kwa kumbadili uraia, Yanga walipata na Hati ya Uhamisho wa
Kimataifa (ITC) ya mchezaji huyo, kutoka Shirikisho la Soka (DRC), na kuwaacha Simba
wakihangaika bila mafanikio kupata ITC ya mchezaji huyo kutoka FERWAFA,
Shirikisho la Soka la Rwanda.
Yanga inamsajili Twite kama mchezaji kutoka St Eloi Lupopo,
klabu ambayo aliichezea kabla ya kutua APR mwaka 2006 kwa pamoja na ndugu yake,
Kabange. Lakini mchezo uliochezwa hapa ni kwamba Twite alikuwa anacheza kwa
mkopo APR.
Habari zaidi zinasema, Yanga inamsajili pia na pacha wake
Mbuyu (pacha wa kuzaliwa kabisa), Kabange, kwa sababu wachezaji hao kawaida yao
kucheza timu moja daima.
Huko nyuma, Yanga iliwahi kuifanyia tena Simba ‘umafia’ kama
huu katika usajili wa wachezaji, Charles Boniface Mkwasa na Yussuf Ismail Bana,
miaka ya 1980.
Simba ilimsaiji beki wa Pamba kama Yussuf Bana, lakini Yanga
wakaingilia kati na kumsajili kwa jina la Yussuf Ismail Bana, Mwenyekiti wa
Chama cha Soka Tanzania (FAT, sasa Shirikisho, TFF), wakati huo Said Hamad El
Maamry akamuidhinisha beki huyo kucheza Yanga.
Simba walijaribu kumuiba kiungo Charles Boniface,
aliyesajiliwa Yanga kutoka Tumbaku ya Morogoro na kumsajili, lakini baadaye
Yanga wakamsajili pia na kumbadili jina, wakimpa Charles Boniface Mkwasa.
Mkwasa alifungiwa na FAT ya El Maamry kabla ya kufunguliwa
baadaye na kuendelea kukipiga Yanga.
Japokuwa kinachozungumzwa kwa sasa ni kwamba, mtoto wa rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ridhiwani Kikwete amewasaidia Yanga
kumbadili njia Mbuyu, lakini uchunguzi wa kina uliofanywa na BIN
ZUBEIRY umegundua mtoto huyo wa Rais Jakaya Mrisho Kikwete hajahusika
kabisa na usajili wa beki huyo, bali ni Bin Kleb.
Kulingana na uzoefu wa ‘fitina za soka ya bongo’,
inawezekana Simba wanamtaja Ridhiwani, ili ionekanane wamemkosa mchezaji huyo
kwa nguvu za vigogo wa serikali, wakati ‘ubabaishaji’ wao wenyewe.
Swali gumu ambalo bado litaendelea kuwaumiza wana Simba ni
kwamba, akijua kwamba mchezaji huyo wakati anamsajili na Yanga pia walikuwa
wanamfukuzia, kwa nini Rage alimuacha Rwanda, ambako Bin Kleb alibaki pia.
Na hiyo inaumiza zaidi inapokumbukwa kwamba beki wao Kevin
Yondan, alisaini na kujiunga na Yanga, wakati tayari akiwa amekwishasaini
kuendelea kuichezea kla bu hiyo- maana yake viongozi wa Simba hawajifunzi
kutoka na makosa.
0 comments:
Post a Comment