• HABARI MPYA

    Wednesday, August 22, 2012

    ULIMWENGU AMETUPA JIBU MAZEMBE WAKO SAHIHI, TFF NI WABABAISHAJI, HATA SAINTFIET AMEGUNDUA


    HATIMAYE mambo yameanza kumnyookea mshambuliaji chipukizi wa kimataifa wa Tanzania, Thomas Emmanuel Ulimwengu baada ya kupandishwa rasmi kwenye kikosi cha kwanza cha klabu ya Tout Puissant Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
    Na Mahmoud Zubeiry
    Ulimwengu alisafiri na Mazembe nchini Misiri kwa ajili ya mechi ya Kundi B ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya wenyeji, Zamalek ya Misri na alikuwa kwenye benchi kwa dakika zote 90 Jumapili wakati wababe hao wa DRC wakiifunga Zamalek mabao 2-1 kwenye Uwanja wa chuo cha Jeshi, Al-Qahirah mjini Cairo.
    Katika mchezo huo ambao, mshambuliaji mwingine chipukizi wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta ‘Sama Goal’ aliifunga Mazembe bao la ushindi dakika ya 44, akiunganisha pasi ya Tressor Mputu Mabi.
    Uli alisajiliwa msimu uliopita Mazembe, lakini kwa muda wote amekuwa kwenye kikosi cha wachezaji wa akiba hadi mwishoni mwa wiki, alipokaa kwenye benchi kwa mara ya kwanza pamoja na kocha Msenegali, Lamine N’Diaye.
    Katika mchezo huo wa Kundi B, Himoonde alitangulia kuifungia Mazembe dakika ya 34 akimalizia pasi ya Mputu, lakini Omotoyossi akaisawazishia Zamalek inayofundishwa na kocha Jorvan Vieira dakika ya 36, pasi ya Mohamed Ibrahim.
    Ushindi huo wa kwanza ugenini kwa Mazembe katika hatua ya makundi, unaifanya TPM ifikishe pointi saba, baada ya kucheza mechi nne, kushinda mbili, sare moja na Berekum Chelsea na kufungwa moja na Al Ahly ugenini.
    Al Ahly iliyotoa sare ya 1-1 na Berekum Chelsea nchini Ghana Jumapili, bado inaongoza kundi hilo kwa pointi zake 10, wakati wababe wapya wa Ghana wanashika nafasi ya tatu kwa pointi zao tano na Zamalek wanashika mkia wakiwa hawana pointi hata moja. 
    Miezi miwili iliyopita, nilifanya mahojiano na Makamu wa Rais wa Mazembe, Mohamed Kamwanya kuhusu kuchelewa kwa Ulimwengu kuingizwa kwenye kikosi cha kwanza, ambaye alisema kwamba mshambuliaji huyo anachelewa kwa sababu kiwango chake bado kidogo.
    Alisema kwamba, Ulimwengu kila anapopewa ruhusa ya kurejea Tanzania kujiunga na timu za taifa, kwanza huchelewa kurudi Lubumbashi na pia hurudi akiwa hayuko fiti.
    “Hicho ndio kinamchelewesha, lakini kama siyo hivyo angekuwa anacheza tu kama mwenzake. Na nyinyi watu wa vyombo vya habari mtusaidie, kwa sababu wachezaji wakija huko wanafanya anasa, wanarudi huku hawako fiti, sasa inakuwa mbaya,”alisema Kamwanya.
    Mazembe ilifikia hatua ya kuwazuia wachezaji wote hao, kurejea Tanzania kujiunga na timu za taifa, kwa sababu hata Samatta inaelezwa anaporejea nyumbani, akirudi Lubumbashi anakuwa ameshuka kiwango.
    Hali hiyo imetafsiriwa inatokana na wachezaji hao kufanya anasa wanapokuwa Dar es Salaam na chanzo ni Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kuchelewa kuwapa tiketi wachezaji hao, wanapomaliza majukumu yao ya kitaifa, hivyo wakati wasubiri tiketi wanaishia kujirusha, kula bata kwa kwenda mbele.
    Kwa kuwa kipindi chote hicho wanakuwa hawafanyi mazoezi na wanaichosha miili yao kwa anasa, wanaporekea Lubumbashi wanampa kazi kocha Lamine N’Diaye kuanza kuwatengeneza upya.
    Amechoka N’Diaye, aliweka ngumu Uli hakurudi nyumbani kuichezea timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 20, Ngorongoro Heroes na kwa kumkosa mpachika mabao wake huyo tegemeo, sisiti kusema ilichangia kwa kiasi kikubwa kutolewa na Nigeria katika mbio za kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Afrika.
    Hilo liliwafanya TFF, walalamike sana hasa baada ya kumpiga stop na Samatta pia kujiunga na kambi ya timu ya taifa ya wakubwa, Taifa Stars kwa ajili ya mchezo wa kirafiki dhidi ya Botswana Jumatano iliyopita, ambao uliisha kwa sare ya 3-3 mjini Gabarone hadi kutishia kulifikisha suala hilo Shirikisho la Soka Afrika (CAF), kwani wamekiuka agizo la Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA).
    Lakini leo TFF, wanasahau kwamba, Mazembe ilikuwa ina hoja na lalamiko la msingi, ambalo naamini kesi hiyo ikienda popote, klabu hiyo bingwa Afrika mara nne, itashinda.
    Mchezaji ni mali ya klabu na kanuni zinatoa mwongozo mzuri juu ya ushiriki wao kwenye timu za taifa, hivyo hata vyama vya soka vina wajibu wa kuzitekeleza kanuni hizo.
    TFF wamezoea kufanya mambo kienyeji na ni jana tu kocha wa Yanga, Mbelgiji Tom Saintefiet aliwalalamikia kwa kumchukua mchezaji wake, Said Bahanuzi akiwa mzima na kumrejesha majeruhi, bila hata ya kutoa taarifa kwa klabu hiyo.
    Tumekwishasau sakata la beki wa Yanga, Stefano Mwasyika kuamua kujitoa timu ya taifa, baada ya kutelekezwa alipoumia hadi klabu yake ikamtibu?
    Bado wamekuwa hawajali hata umuhimu wa kuwarejesha mapema wachezaji wa nje baada ya kumaliza majukumu yao ya kitaifa.
    Ndiyo maana ninasema, kabla ya kuwahukumu Mazembe, tunapaswa kutafuta kiini cha ghafla mabingwa hao wa zamani Afrika kupuuza wito wa TFF kutuma wachezaji Dar es Salaam.
    Mara kadhaa nimekuwa nikiwaona makocha wa nchi jirani, ambazo wachezaji wake wanacheza hapa Tanzania wakija nchini kuwafuatilia wachezaji wao, mfano Mserbia Milutin Sredojevic ‘Micho’ wa Rwanda au Msoctland, Bobby Williamson wa Uganda.
    Wanapokuwa hapa hujionea wachezaji wao namna wanavyocheza na kufanya uteuzi kwa ajili ya timu taifa, juu ya wachezaji ambao wanawajua fika. Micho anakwenda hatua kadhaa zaidi, anawahangaikia wachezaji wa Rwanda kupata timu Ulaya, au nchi nyingine Afrika, ambako watakusanya uzoefu zaidi na baadaye kuisaidia Amavubi.
    Lakini sijawahi kusikia hata siku moja kocha wa timu ya taifa, si Kim Poulsen tu, tangu Mdenmark mwingine, Jan Poulsen aliyemrithi Marcio Maximo kutoka Brazil akisafiri kwenda DRC kuwafuatilia Samatta na Ulimwengu, ama Kenya ambako katika Ligi Kuu tuna mtu anaitwa Idrisa Rajab au Angola ambako tuna mtu anaitwa Said Maulid.
    Huwezi kuniambia eti leo SMG ana uzee wa kutelekezwa moja kwa moja timu ya taifa bila kuzingatia uwezo wake unaomuweka katika moja ya ligi kubwa Afrika, Girabola, wakati mwaka 2000 mchezaji huyo akisajiliwa Simba SC kutoka Kigoma, Shaaban Nditi alikuwa anacheza Singida United Ligi Kuu tangu 1999 na akina Kipanya Malapa na Edward Rodgers Kayoza.
    Wakati fulani, Jan Poulsen alikwenda Sweden kumfuatilia Athumani Machuppa, kwa kuwa ni pua na mdomo na kwao Denmark- lakini zaidi makocha wa Taifa Stars wamekuwa na desturi ya kusubiri sifa za wachezaji kupitia vyombo vya habari ndipo wawaite, ndio maana historia inamtaja Amy Ninje kama mmoja wa wachezaji wa zamani wa Taifa Stars.
    Baada ya mechi ya kwanza dhidi ya Nigeria, Flying Eagles, kocha wa Ngorongoro Heroes, Mdenmark Jakob Michelsen alisema kwamba ataongeza nguvu katika kikosi chake kwa kumuita kiungo Adam Nditi wa Chelsea ya vijana ya England, ambaye tayari ameingia kwenye programu za kukomazwa kwenye kikosi cha wakubwa cha mabingwa hao wa Ulaya.
    Sijui jitihada gani za dhati zilifanyika- lakini nachokiona hapa kocha anatakiwa kusafiri hadi London na kufika Stamford Bridge kukutana na makocha wa Nditi kuzungumza nao kuhusu huyo mchezaji na kuzungumza naye mchezaji mwenyewe pia, kuliko kuzungumza kwenye vyombo vya habari.
    TFF inapaswa kumpa fungu hata Kim akafuatilie na kujua kuhusu Nditi kama yupo kwenye nafasi ya kuchezea Tanzania, kulikoni kuamua kwa kudhani tukiwa hapa nyumbani.
    Sasa baada ya kumzuia Uli kurudi Tanzania, ndani ya wiki mbili amepandishwa kikosi cha kwanza cha Mazembe na kukaa benchi katika mechi ya Ligi ya Mabingwa- ina maana mwezi ujao sasa tutakuwa tunazungumza habari nyingine kuhusu mchezaji huyu.
    Kufanya vizuri kwa wachezaji hawa ni faida kwa Tanzania pia- na kuwakwamisha kufanya vizuri ni hasara zaidi kwa Mazembe, iliyowekeza fedha nyingi kwa nyota hawa, ingawa na taifa letu pia litapoteza.
    TFF kwao kupoteza si hasara ndio maana hawakujutia Mwasyika alipovunjika goti na hawakujali Athumani Iddi ‘Chuji’ alipopoteza mwelekeo, ndiyo maana hawakumsaidia, ingawa leo akiwa amerudi mstarini, ndio wanaona umuhimu wake.
    Sasa wakati TFF wakilialia Dar es Salaam na kupigia mikwara ya kwenda CAF na FIFA kushitaki, Ulimwengu ametupa jibu Mazembe walikuwa sahihi.  
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: ULIMWENGU AMETUPA JIBU MAZEMBE WAKO SAHIHI, TFF NI WABABAISHAJI, HATA SAINTFIET AMEGUNDUA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top