• HABARI MPYA

    Saturday, August 11, 2012

    SIRI YA SIMBA KUMPOTEZA TWITE YACHIFUKA

    Mbuyu Twite

    Na Mahmoud Zubeiry
    MAMBO matatu yamemfanya beki Mbuyu Twite wa APR ya Rwanda, aachane na Simba SC na kuamua kujiunga na Yanga SC, BIN ZUBEIRY imebaini baada ya uchunguzi wa kina uliohusisha vyanzo kutoka Tanzania, Rwanda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
    Mambo hayo ambayo kwa mjumuisho unaweza kuyaita ‘Ujanja ujanja wa mjini’ wa viongozi wa klabu hiyo ndio leo, yanaiponza klabu hiyo kumpoteza aina ya mchezaji ambaye walimuhitaji sana kwenye kikosi chao ili kujiimarisha.
    Mosi; Namna ambavyo ‘walimuenzi’ kiungo Patrick Mutesa Mafisango (sasa marehemu), pili; desturi ya kuwaacha wachezaji wa kigeni baada ya kuwasajili, hata kabla hawajaitumikia timu mfano Lino Masombo, Derrick Walullya na wengineo na tatu hadhi ya klabu yao kwa sasa ukilinganisha Yanga na Azam FC.
    Habari za kiuchunguzi, ambazo BIN ZUBEIRY imezipata zinasema kwamba Mbuyu alilishwa ‘sumu’ za kutosha ili aichukie Simba, kwanza klabu hiyo ilivyoutelekeza mwili wa marehemu Mafisango baada ya kifo chake, ambao hakuna kiongozi mkuu wa klabu hjiyo hata mmoja aliyekwenda kumzika DRC, zaidi ya Mjumbe mmoja wa Kamati ya Utendaji na mchezaji mmoja.
    Pamoja na namna ambavyo Simba hawakujali kabisa mambo mengine muhimu kuhusu marehemu Mafisango, kama arobaini yake na kadhalika, Wakongo wameichukulia hiyo kama ni dharaua na ulipotokea mjadala Mbuyu aende wapi, watu wa Kongo wakamnyooshea kidole kinachoelekeza Jangwani.
    Ikumbukwe, Mafisango aliyejiunga na Simba akitokea Azam FC, iliyomsajili kutoka APR ya Rwanda, alifariki akiwa mchezaji muhimu ndani ya Simba akiongoza kwa kufunga mabao na mwenye mchango mkubwa kwenye timu.
    Simba, hivi karibuni ilimsajili mchezaji Lino Masombo kutoka DRC, lakini baada ya mwezi mmoja na ushei ikamtema kama ilivyofanya kwa Mganda, Derrick Walullya msimu uliopita, hilo limetajwa kumsitisha Mbuyu kuangukia Msimbazi na kuamua kurudisha fedha zote alizochukua kwa Mwenyekiti, Ismail Aden Rage (dola za kimarekani 30,000 kwa mujibu wa Simba).
    Lakini pia, wakati Mbuyu anasaini Simba kuchukua fedha, alikuwa hajui kwamba katika soka ya Tanzania hivi sasa, klabu ambazo zinachuana kwa ‘utajiri’ ni Yanga, ambao Mwenyekiti wao Yussuf Manji ni mfanyaiashara mkubwa na Azam FC ambayo inamilikiwa na mfanyabiashara mwingine, Said Salim Bakhresa.
    Yanga imemsajili Twite, wakati tayari akiwa amekwishaini Simba SC, baada ya kumrudisha kwenye uraia wake wa asili, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), badala ya Rwanda aliopewa wakati akicheza nchini humo na kumbadili jina pia.
    Kwa kumbadili uraia, Yanga walipata na Hati ya Uhamisho wa Kimataifa (ITC) ya mchezaji huyo, kutoka Shirikisho la Soka (DRC), na kuwaacha Simba wakihangaika bila mafanikio kupata ITC ya mchezaji huyo kutoka FERWAFA, Shirikisho la Soka la Rwanda. 
    Yanga inamsajili Twite kama mchezaji kutoka St Eloi Lupopo, klabu ambayo aliichezea kabla ya kutua APR mwaka 2006 kwa pamoja na ndugu yake, Kabange. Lakini mchezo uliochezwa hapa ni kwamba Twite alikuwa anacheza kwa mkopoAPR.
    Habari zaidi zinasema, Yanga inamsajili pia na pacha wake Mbutu (pacha wa kuzaliwa kabisa), Kabange, kwa sababu wachezaji hao kawaida yao kucheza timu moja daima.
    Huko nyuma, Yanga iliwahi kuifanyia tena Simba ‘umafia’ kama huu katika usajili wa wachezaji, Charles Boniface Mkwasa na Yussuf Ismail Bana, miaka ya 1980.
    Simba ilimsaiji beki wa Pamba kama Yussuf Bana, lakini Yanga wakaingilia kati na kumsajili kwa jina la Yussuf Ismail Bana, Mwenyekiti wa Chama cha Soka Tanzania (FAT, sasa Shirikisho, TFF), wakati huo Said Hamad El Maamry akamuidhinisha beki huyo kucheza Yanga.
    Simba walijaribu kumuiba kiungo Charles Boniface, aliyesajiliwa Yanga kutoka Tumbaku ya Morogoro na kumsajili, lakini baadaye Yanga wakamsajili pia na kumbadili jina, wakimpa Charles Boniface Mkwasa.
    Mkwasa alifungiwa na FAT ya El Maamry kabla ya kufunguliwa baadaye na kuendelea kukipiga Yanga.
    Japokuwa kinachozungumzwa kwa sasa ni kwamba, mtoto wa rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ridhiwani Kikwete amewasaidia Yanga kumbadili njia Mbuyu, lakini uchunguzi wa kina uliofanywa na BIN ZUBEIRY umegundua mtoto huyo wa Rais Jakaya Mrisho Kikwete hajahusika kabisa na usajili wa beki huyo, bali ni Bin Kleb.
    Kulingana na uzoefu wa ‘fitina za soka ya bongo’, inawezekana Simba wanamtaja Ridhiwani, ili ionekanane wamemkosa mchezaji huyo kwa nguvu za vigogo wa serikali, wakati ‘ubabaishaji’ wao wenyewe.
    Swali gumu ambalo bado litaendelea kuwaumiza wana Simba ni kwamba, akijua kwamba mchezaji huyo wakati anamsajili na Yanga pia walikuwa wanamfukuzia, kwa nini Rage alimuacha Rwanda, ambako Bin Kleb alibaki pia.
    Na hiyo inaumiza zaidi inapokumbukwa kwamba beki wao Kevin Yondan, alisaini na kujiunga na Yanga, wakati tayari akiwa amekwishasaini kuendelea kuichezea kla bu hiyo- maana yake vipongozi wa Simba hawajifunzi kutoka na makosa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SIRI YA SIMBA KUMPOTEZA TWITE YACHIFUKA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top