• HABARI MPYA

    Monday, May 08, 2017

    MBEYA CITY HAITAKI KUWA NGAZI YA UBINGWA YANGA

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MBEYA City haitaki kuwa ngazi ya ubingwa kwa Yanga SC na imesema na Jumamosi ijayo patachimbika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
    Akizungumza na Bin Zubeiry Sports – Online jana kwa simu kutoka Mbeya, Meneja wa Mbeya, Geoffrey Katepa alisema kwamba wamekuwa katika maandalizi mazuri kuelekea mchezo huo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    Katepa alisema kwamba kikosi cha MCC kimerejea jana tu mjini Mbeya kutoka Sumbawanga, ambako kilikuwa kimeweka kambi ya siku tano iliyohusisha pia michezo minne ya kirafiki, ambayo walishinda yote.
    “Tumerudi hapa Mbeya na tunaendelea na mazoezi makali kwa ajili ya maandalizi yetu ya mwisho mwisho kabla ya kwenda Dar es Salaam,”alisema Katepa, kiungo wa zamani wa Yanga.
    Katepa amesema kwamba wanajiandaa vizuri ili wakaifunge Yanga mjini Dar es Salaam na kujenga heshima dhidi ya mabingwa hao watetezi.
    “Sisi tunachotaka ni kuwafunga tu, haijalishi kama hatuwi mabigwa au hatushuki. Tunataka heshima tu, na kuwafunga mabingwa watetezi itakuwa heshima nzuri. Kikubwa sisi hatutaki kuwa ngazi ya ubingwa ya Yanga,”alisema.
    Kabla ya kumenyana na MCC Jumamosi, kesho Yanga SC watateremka Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kumenyana na Kagera Sugar ya Bukoba katika mchezo mwingine wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: MBEYA CITY HAITAKI KUWA NGAZI YA UBINGWA YANGA Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top