• HABARI MPYA

    Friday, April 14, 2017

    SAMATTA NA GENK WAPIGANA KIUME ULAYA, WAPIGWA 3-2 UGENINI

    Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
    MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta usiku wa jana amecheza dakika zote 90 timu yake, KRC Genk ikifungwa mabao 3-2 ugenini katika mchezo wa kwanza wa Robo Fainali ya UEFA Europa League dhidi ya wenyeji, Celta Vigo Alhamisi Uwanja wa Balaidos.  
    Samatta jana alikuwa chini ya ulinzi mkali wa mabeki wa CeltaVigo, lakini wakasahau kwamba Genk ina wakali wengine wenye uwezo wa kufunga.
    Mabao ya Celta Vigo yalifungwa na kiungo Mdenmark mzaliwa wa Uganda, Pione Sisto dakika ya 15, Iago Aspas dakika ya 17 na John Guidetti dakika ya 38, wakati ya Genk yalifungwa na Jean-Paul Boetius dakika ya 10 na Thomas Buffel dakika ya 67.  
    Kwa matokeo hayo, Genk watajitaji ushindi wa 1-0 tu kwenye mchezo wa marudiano Genk wiki ijayo ili kwenda Nusu Fainali.
    Mchezo wa jana ulikuwa wa 51 kwa Samatta tangu ajiunge na Genk Januari mwaka jana akitokea TP Mazembe ya DRC akiwa amefunga mabao 18.
    Kati ya mechi hizo 51, michezo 18 Samatta alicheza msimu uliopita na 32 msimu huu na kati ya hiyo, ni michezo 31 tu ndiyo alianza, 10 msimu uliopita na 21 msimu huu.
    Mechi 19 kati ya hizo alitokea benchi, nane msimu uliopita na 11 msimu huu, wakati 11 hakumaliza baada ya kutolewa, tano msimu uliopita na sita msimu huu na katika mabao hayo 18, 12 amefunga msimu huu na sita msimu uliopita.
    Celta de Vigo : Alvarez, Mallo, Fontas, Radoja, Hernandez, Guidetti/Beauvue dk55, Aspas, Sisto, Wass/Jozabed dk79 na Jonny Cabral.
    KRC Genk: Ryan, Uronen, Colley, Brabec, Castagne, Berge, Malinovskyi/Heynen dk90+2, Pozuelo, Trossard/Writers dk83, Boetius/Buffalo dk61 na Samatta.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SAMATTA NA GENK WAPIGANA KIUME ULAYA, WAPIGWA 3-2 UGENINI Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top