• HABARI MPYA

    Tuesday, October 01, 2013

    HABARI NJEMA SIMBA SC, MAJERUHI KARIBU WOTE HADI HENRY JOSEPH NA CHOLLO WAANZA MAZOEZI LEO

    Na Princess Asia, IMEWEKWA OKTOBA 1, 2013 SAA 5:29 ASUBUHI
    HABARI njema kwa wapenzi wa Simba SC. Wachezaji karibu wote waliokuwa majeruhi katika timu hiyo leo wameanza mazoezi na waliobaki wanaugulia maumivu yao ni wawili tu.
    Daktari wa Simba SC, Yassin Gembe ameiambia BIN ZUBEIRY leo kwamba, kiungo Amri Kiemba aliyeumia nyama katika mchezo dhidi ya JKT Ruvu Jumapili, leo amefanya mazoezi mepesi.  
    “Kwa kweli Kiemba hajaumia sana, ni maumivu madogo, ambayo atakuwa anaendelea na tiba pamoja na mazoezi na leo pia amefanya mazoezi na hakuna shaka atacheza mechi ijayo,”alisema Gembe, aliyetua Simba SC akitokea Mtibwa Sugar msimu huu.
    Gembe alisema majeruhi wengine wote, mabeki Issa Rashid ‘Baba Ubaya’, Nassor Masoud ‘Chollo’, kiungo Henry Joseph na mshambuliaji Zahor Pazi nao wamefanya mazoezi leo.
    Wachezaji pekee wawili ambao wanaendelea kuugulia ni ni beki Miraj Adam na kiungo Abdallah Seseme, ambao wote wamefungwa ‘hogo’. Wachezaji hao waliopandishwa kutoka Simba B walikuwa wana wiki nne za kuwa nje na sasa wamebakiza wiki mbili kila mmoja.
    Nahodha wa Simba SC, Nassor Masoud ''Chollo' wa pili kulia ameanza mazoezi

    “Kwa hiyo maana yake baada ya wiki mbili nyingine, watakuwa na wiki mbili za mazoezi ili kuwa fiti na baada ya hapo watakuwa tayari kuanza kucheza,”alisema Gembe.
    Simba SC inayoongoza Ligi Kuu kwa pointi zake 14 baada ya mechi sita, itashuka tena dimbani Jumamosi kumenyana na Ruvu Shooting, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. 
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: HABARI NJEMA SIMBA SC, MAJERUHI KARIBU WOTE HADI HENRY JOSEPH NA CHOLLO WAANZA MAZOEZI LEO Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top