KIPA namba mbili wa klabu ya Simba ya Dar es Salaam, Ally
Mustafa Mtinge ‘Barthez’ amesaini Yanga, wakati Shaaban Hassan Kado anarudishwa
Mtibwa Sugar katika mkataba wa kubadilishana wachezaji baina ya timu hizo mbili.
Chanzo cha habari kutoka Yanga, kimeiambia BIN ZUBEIRY kwamba, mbali na
Barthez (pichani kushoto) Yanga pia imesajili wachezaji wengine watatu hadi sasa, beki wa kulia Juma
Abdul kutoka Mtibwa Sugar, beki wa kushoto David Luhende kutoka Kagera Sugar,
beki wa kati Kelvin Yondan kutoka Simba na kiungo Nizar Khalfan aliyekuwa
anacheza Marekani.
Usajili huu, shukrani kwao, wagombea uongozi katika uchaguzi
wa Yanga, unaotarajiwa kufanyika Julai 15, mwaka huu- Yussuf Manji anayewania Uenyekiti
na Abdallah Ahmad Bin Kleb anayewania Ujumbe pamoja na mwanachama wa klabu
hiyo, ambaye hagombei nafasi yoyote, Seif Ahmed ‘Magari’.
Aidha, Yanga bado inaendelea na mazungumzo na wachezaji
wawili, beki Juma Said Nyosso wa Simba na mshambuliaji Danny Davis Mrwanda
aliyekuwa anacheza Dong Tam Long An ya Vietnam.
Hakuna zengwe kuhusu Mrwanda- ila Nyosso, baadhi ya wadau wa
Yanga, wanasema ni Simba damu, wakati pia klabu hiyo imepanga kutosajili zaidi wachezaji
wa mahasimu wao wa jadi, zaidi ya Yondan na Barthez.
BIN ZUBEIRY inajua, juhudi za Yanga kumpata mshambuliaji wa kimataifa wa
Uganda, Owen Kasuule zimegonga ukuta baada ya mchezaji huyo kusaini El Merreikh
ya Sudan. “Kasuule ametuambia amesaini El Merreikh, nasi tumeachana naye,”kilisema
chanzo kutoka Yanga.
Lakini Yanga bado inaendelea na jitihada za kumsajili
mshambuliaji wa kimataifa wa Rwanda, Meddie Kagere, wakati kutoka kikosi cha
msimu uliopita, wachezaji watatu wa kigeni, kipa Yaw Berko na washambuliaji
Kenneth Asamoah wote kutoka Ghana watatemwa sambamba na Davies Mwape kutoka
Zambia.
Hivi sasa Yanga inaumiza kichwa kupata beki wa kati kutoka nje
ya Tanzania atakayekuwa akisaidiana kazi na Nadir Haroub ‘Cannavaro’ na Yondan.
Aidha, Yanga inafuatilia kama kweli kiungo mkabaji, Shaaban Mussa Nditi
amesaini Coastal Union ya Tanga au la ili ijaribu kumsajili.
Wachezaji wengine ambao Yanga inawatolea macho ni nyota wa
Mtibwa Sugar Said Bahanuzi ‘Ortega’ na Hussein Javu- ambao wote wana mikataba na
timu hiyo ya Manungu.
Tayari kutoka kikosi cha msimu uliopita wachezaji wazawa
Nsajigwa Shadrack, Kiggi Makassy, Bakari Mbega, Abuu Ubwa na Zuberi Ubwa
wamekwishatemwa.
0 comments:
Post a Comment