• HABARI MPYA

    Thursday, June 07, 2012

    BREAKING NEWS: YANGA YAIBOMOA TENA SIMBA, USAJILI JANGWANI 80% MWAAAA!


    KIPA namba mbili wa klabu ya Simba ya Dar es Salaam, Ally Mustafa Mtinge ‘Barthez’ amesaini Yanga, wakati Shaaban Hassan Kado anarudishwa Mtibwa Sugar katika mkataba wa kubadilishana wachezaji baina ya timu hizo mbili.
    Chanzo cha habari kutoka Yanga, kimeiambia BIN ZUBEIRY kwamba, mbali na Barthez (pichani kushoto) Yanga pia imesajili wachezaji wengine watatu hadi sasa, beki wa kulia Juma Abdul kutoka Mtibwa Sugar, beki wa kushoto David Luhende kutoka Kagera Sugar, beki wa kati Kelvin Yondan kutoka Simba na kiungo Nizar Khalfan aliyekuwa anacheza Marekani.
    Usajili huu, shukrani kwao, wagombea uongozi katika uchaguzi wa Yanga, unaotarajiwa kufanyika Julai 15, mwaka huu- Yussuf Manji anayewania Uenyekiti na Abdallah Ahmad Bin Kleb anayewania Ujumbe pamoja na mwanachama wa klabu hiyo, ambaye hagombei nafasi yoyote, Seif Ahmed ‘Magari’.
    Aidha, Yanga bado inaendelea na mazungumzo na wachezaji wawili, beki Juma Said Nyosso wa Simba na mshambuliaji Danny Davis Mrwanda aliyekuwa anacheza Dong Tam Long An ya Vietnam.
    Hakuna zengwe kuhusu Mrwanda- ila Nyosso, baadhi ya wadau wa Yanga, wanasema ni Simba damu, wakati pia klabu hiyo imepanga kutosajili zaidi wachezaji wa mahasimu wao wa jadi, zaidi ya Yondan na Barthez.
    BIN ZUBEIRY inajua, juhudi za Yanga kumpata mshambuliaji wa kimataifa wa Uganda, Owen Kasuule zimegonga ukuta baada ya mchezaji huyo kusaini El Merreikh ya Sudan. “Kasuule ametuambia amesaini El Merreikh, nasi tumeachana naye,”kilisema chanzo kutoka Yanga.
    Lakini Yanga bado inaendelea na jitihada za kumsajili mshambuliaji wa kimataifa wa Rwanda, Meddie Kagere, wakati kutoka kikosi cha msimu uliopita, wachezaji watatu wa kigeni, kipa Yaw Berko na washambuliaji Kenneth Asamoah wote kutoka Ghana watatemwa sambamba na Davies Mwape kutoka Zambia.
    Hivi sasa Yanga inaumiza kichwa kupata beki wa kati kutoka nje ya Tanzania atakayekuwa akisaidiana kazi na Nadir Haroub ‘Cannavaro’ na Yondan. Aidha, Yanga inafuatilia kama kweli kiungo mkabaji, Shaaban Mussa Nditi amesaini Coastal Union ya Tanga au la ili ijaribu kumsajili.
    Wachezaji wengine ambao Yanga inawatolea macho ni nyota wa Mtibwa Sugar Said Bahanuzi ‘Ortega’ na Hussein Javu- ambao wote wana mikataba na timu hiyo ya Manungu.
    Tayari kutoka kikosi cha msimu uliopita wachezaji wazawa Nsajigwa Shadrack, Kiggi Makassy, Bakari Mbega, Abuu Ubwa na Zuberi Ubwa wamekwishatemwa.
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: BREAKING NEWS: YANGA YAIBOMOA TENA SIMBA, USAJILI JANGWANI 80% MWAAAA! Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top