• HABARI MPYA

    Monday, April 03, 2017

    SERENGETI BOYS YALAZIMISHA SARE KWA GHANA 2-2

    Na Rehema Lucas, DAR ES SALAAM
    TIMU ya soka ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys imelazimishwa sare ya kufungana mabao 2-2 na Ghana katika mchezo wa kirafiki uliofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam jioni ya leo.
    Huo ulikuwa mchezo wa tatu wa majaribio katika maandalizi ya Serengeti Boys kwenda Gabon kwenye fainali za Afrika za U-17 mwezi Mei baada ya awali kuifunga Burundi 3-0 na 2-0 mjini Bukoba wiki iliyopita.
    Ghana walitangulia kwa mabao mawili ya Sulley Ibrahimu dakika ya 30 na Arko Mensah dakika ya 73, kabla ya Tanzania kusawazisha kupitia kwa Asad Juma kwa penalti na Muhsin Malima mabao yote yakifungwa dakika za nyongeza baada ya kutimu dakika 90 za kawaida za mchezo.
    Beki wa Ghana, Yusif Abdulrazak akibinuka kuondosha mpira kwenye himaya ya Yohana Nkomola wa Tanzania leo

    Mapema kabla ya mchezo huo, Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe aliwakabidhi Serengeti Boys bendera tayari kwa safari ya Morocco Jumatano kwenda kuweka kambi ya mwezi mmoja kujiandaa na fainali za AFCON U-17 nchini Gabon.
    Kikosi cha Tanzania; Ramadhani Kabwili, Ally Msengi, Israel Mwenda, Nickson Kibabage, Dickson Job, Ally Ng'anzi, Asad Juma, Shaaban Zubeiry, Yohana Nkomola, Kevin Naftal na Abdallah Rashid. 
    Ghana; Ibrahim Danlad, Ayiah Eric, Yakubu Najeeb, Alhassan Rashid, Osman Faisal, Yusif Abdulrazak, Owusu Bismarck Terry, Antwi Nana Kamwe, Levesh Gabriel, Sulley Ibrahim na Toku Emmanuel.          
    • Blogger Comments
    • Facebook Comments

    0 comments:

    Item Reviewed: SERENGETI BOYS YALAZIMISHA SARE KWA GHANA 2-2 Rating: 5 Reviewed By: Mahmoud Bin Zubeiry
    Scroll to Top